Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 40:20-32 Biblia Habari Njema (BHN)

20. Kisha, yule mtu akapima urefu na upana wa lango la upande wa kaskazini wa ua wa nje.

21. Kulikuwa na vyumba vitatu vya walinzi kila upande wa lango, vipimo vya miimo yake na matao yake vilikuwa kama vile vya lango la kwanza. Urefu wote wa ile njia ulikuwa kwa jumla mita 25 na upana wake mita kumi na mbili u nusu.

22. Chumba cha kuingilia na madirisha na matao yake, pia ile mitende iliyochorwa ukutani, vyote vilifanana na vile vya lango la mashariki. Hapo palikuwa na ngazi saba za kupandia kwenye lango, na matao yake yalikuwa mbele yake.

23. Kutoka hapo penye njia ya kuingilia ya kaskazini na kuvuka huo ua moja kwa moja kulikuwa na njia nyingine ya kuingilia iliyoelekea kwenye ua wa ndani, kama ilivyokuwa upande wa mashariki. Yule mtu alipima urefu wa kutoka njia mpaka njia, akapata mita 50.

24. Yule mtu akanichukua upande wa kusini; huko nako kulikuwako lango; alipima miimo yake na ukumbi na vipimo vyake vilikuwa sawa na miimo na kumbi nyingine.

25. Kulikuwa na madirisha pande zote kama ilivyokuwa katika vyumba vingine. Urefu wake ulikuwa mita 25 na upana wake mita kumi na mbili u nusu.

26. Kulikuwa na ngazi saba za kupandia kwenye njia hiyo ya kuingilia na mwishoni mwake kulikuwa na ukumbi uliokuwa mkabala na ua. Kulikuwa na michoro ya mitende kwenye kuta za ndani zilizokuwa mkabala na hiyo njia ya kuingilia.

27. Mkabala na njia hiyo ya kuingilia kulikuwa na njia ya kuingilia kwenye ua wa ndani. Yule mtu akapima urefu kati ya hizo njia, akapata mita 50.

28. Yule mtu akanipitisha kwenye njia ya kuingilia upande wa kusini, tukafika kwenye ua wa ndani. Aliipima hiyo njia nayo ilikuwa sawa na zile njia nyingine za kuingilia kwenye kuta za nje.

29. Vyumba vya walinzi, ukumbi, na kuta zake vilikuwa na ukubwa uleule kama vile vingine; kulikuwa na madirisha pia kandokando ya hiyo njia ya kuingilia na kwenye ukumbi. Ilikuwa na urefu mita 25 na upana mita kumi na mbili u nusu.

30. Kulikuwa na vyumba kandokando ya hiyo njia ya kuingilia, vikiwa na urefu wa mita 25 na upana wake mita kumi na mbili u nusu.

31. Ule ukumbi ulikuwa mkabala na ua wa nje. Na kulikuwa na michoro ya mitende kwenye nguzo kandokando ya hiyo njia ya kuingilia kwenye ngazi. Kulikuwa na ngazi nane za kupandia lango hili.

32. Yule mtu alinipeleka upande wa mashariki wa ua wa ndani. Akaipima ile njia ya kuingilia, nayo ilikuwa na urefu kama zile njia nyingine za kuingilia.

Kusoma sura kamili Ezekieli 40