Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 39:16-29 Biblia Habari Njema (BHN)

16. Huko kutakuwa pia mji utakaoitwa Hamona. Ndivyo watakavyoisafisha nchi.

17. “Sasa, ewe mtu, mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Waite ndege wote na wanyama wote wa porini wakusanyike toka pande zote na kuja kula karamu ya kafara ninayowaandalia, ambayo itakuwa kubwa sana juu ya milima ya Israeli, ambako watakula nyama na kunywa damu.

18. Watakula nyama ya mashujaa, watakunywa damu ya wakuu wa dunia watakaochinjwa kama kondoo madume au wanakondoo, mbuzi au mafahali wanono wa Bashani.

19. Katika karamu hiyo ninayowafanyia watakula mafuta na kushiba. Watakunywa damu na kulewa.

20. Mezani pangu, watashibishwa kwa farasi, wapandafarasi, mashujaa na watu wote wa vita. Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nimesema.”

21. Mwenyezi-Mungu aliniambia, “Nitayafanya mataifa yote yauone utukufu wangu, na kuwaonesha jinsi ninavyotumia nguvu yangu kutekeleza hukumu zangu za haki.

22. Waisraeli watajua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu, Mungu wao, tangu siku hiyo na baadaye.

23. Mataifa yatajua kuwa Waisraeli walikwenda uhamishoni kutokana na makosa yao wenyewe waliyonikosea. Waliniasi, nami nikageuka wasinione, nikawaweka mikononi mwa maadui zao wakauawa.

24. Niligeuka wasinione, nikawatenda kulingana na uchafu na makosa yao.

25. “Kwa hiyo mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Sasa nitawahurumia Waisraeli wazawa wa Yakobo, na kuwarudishia fanaka yao. Daima nataka jina langu takatifu liheshimiwe.

26. Watakapokuwa wanaishi kwa usalama katika nchi yao, bila ya kutishwa, watasahau aibu yao na uasi walionitenda.

27. Wakati huo, nitakuwa nimewarudisha kutoka kwa mataifa na kuwakusanya kutoka nchi za maadui zao na kudhihirisha utakatifu wangu mbele ya mataifa mengi.

28. Kisha watatambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu, Mungu wao, kwa sababu mimi niliwapeleka uhamishoni kati ya mataifa na kuwarudisha tena katika nchi yao. Sitamwacha hata mtu wao abaki miongoni mwa mataifa.

29. Nitakapowamiminia Waisraeli roho yangu, sitageuka tena wasinione. Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nimesema.”

Kusoma sura kamili Ezekieli 39