Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 38:1-8 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Neno la Mwenyezi-Mungu lilinijia:

2. “Wewe mtu! Mgeukie Gogu mfalme wa nchi ya Magogu ambaye ni mtawala mkuu wa Mesheki na Tubali.

3. Toa unabii juu yake na kumwambia kuwa mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Mimi nitapambana nawe ewe Gogu mtawala wa Mesheki na Tubali.

4. Mimi nitakuzungusha na kukutia ndoana matayani mwako, na kukutoa nje wewe pamoja na jeshi lako lote: Farasi na wapandafarasi na kundi kubwa la watu wamevaa mavazi ya vita, ngao na vigao mikononi, wanapunga mapanga yao.

5. Wanajeshi kutoka Persia, Kushi na Puti wako pamoja nao; wote wana ngao na kofia za chuma.

6. Pia vikosi kutoka Gomeri, Beth-togarma, upande wa kaskazini kabisa, na majeshi yao yote pamoja na majeshi kutoka mataifa mengine, yako pamoja nawe.

7. Jitayarishe, ukae wewe mwenyewe na jeshi lako lote pamoja na wengine wote ulio nao, ukawalinde.

8. “Baada ya siku nyingi utaitwa kuishambulia nchi ambayo watu wengi waliletwa kutoka mataifa mengi na sasa wanaishi bila vitisho vya vita. Utaishambulia milima ya Israeli ambayo hapo awali ilikuwa jangwa na mahame kwa muda mrefu, lakini sasa watu wote huko wanaishi kwa usalama.

Kusoma sura kamili Ezekieli 38