27. Lakini mtu mwovu akiachana na uovu aliofanya, akatenda mambo yaliyo haki na sawa, huyo atayaokoa maisha yake.
28. Kwa kuwa amefikiri, akaachana na makosa aliyoyafanya, hakika ataishi; hatakufa.
29. Lakini nyinyi Waisraeli mwasema, ‘Anachotenda Mwenyezi-Mungu si sawa!’ Enyi Waisraeli, je, ninachofanya mimi si sawa? Mnachofanya nyinyi ndicho kisicho sawa.
30. “Kwa hiyo, mimi Bwana Mwenyezi-Mungu, nasema hivi: Nitawahukumu nyinyi Waisraeli, kila mmoja wenu, kulingana na mwenendo wake. Tubuni na kuachana na makosa yenu, yasije yakawaangamiza.
31. Tupilieni mbali dhambi mlizonitendea; jipatieni moyo na roho mpya. Enyi Waisraeli, ya nini mfe?
32. Sifurahii kifo cha mtu yeyote. Hivyo tubuni ili mpate kuishi. Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nimesema.”