Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 12:9-20 Biblia Habari Njema (BHN)

9. “Wewe mtu! Je, hao waasi wa Israeli hawajakuuliza maana ya hicho ulichofanya?

10. Waambie kuwa mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema: Kauli hii yangu yahusu mambo yatakayompata mtawala wa Yerusalemu na watu wote wa Israeli wanaoishi humo.

11. Waambie kuwa wewe ni ishara kwao; kama ulivyofanya ndivyo itakavyotendeka kwao: Watakwenda uhamishoni; naam, watachukuliwa mateka.

12. Naye mtawala wao atajitwika mzigo wake mabegani wakati wa usiku, atatoka kupitia ukuta atakaotoboa apate kutoka; atafunika uso wake ili asiione nchi kwa macho yake.

13. Lakini nitatandaza wavu wangu juu yake, naye atanaswa katika mtego wangu. Nitampeleka Babuloni, nchi ya Wakaldayo; naye akiwa huko atakufa bila kuiona hiyo nchi.

14. Wafuasi wake wote, washauri wake na vikosi vyake vyote, nitawatawanya nje kila upande. Nitauchomoa upanga na kuwafuatilia nyuma.

15. Nitakapowatawanya kati ya mataifa mengine na nchi za mbali, ndipo watakapotambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu.

16. Lakini nitawaacha wachache waokoke vitani, wanusurike njaa na maradhi mabaya; ili hao waweze kuwasimulia watu wa mataifa wanamoishi jinsi walivyotenda mabaya. Ndipo watakapotambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu.”

17. Neno la Mwenyezi-Mungu likanijia:

18. “Wewe mtu, kula chakula na kunywa maji yako ukitetemeka kwa hofu.

19. Waambie watu wa nchi hii, kuwa mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema juu ya wakazi wa Yerusalemu ambao bado wamo nchini Israeli, kwamba watakula chakula chao kwa hofu na watakunywa maji yao kwa kufadhaika, kwani nchi yao haitakuwa na kitu, kwa sababu kila mkazi ni mdhalimu.

20. Miji yenye watu itateketezwa, na nchi itakuwa ukiwa. Nanyi mtatambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu.”

Kusoma sura kamili Ezekieli 12