Agano la Kale

Agano Jipya

Danieli 8:8-26 Biblia Habari Njema (BHN)

8. Hapo yule beberu alijikweza sana. Lakini alipofikia kilele cha nguvu zake, ile pembe yake kubwa ikavunjika. Badala yake zikaota pembe nne zilizoonekana waziwazi, zikiwa zimeelekea pande nne za pepo.

9. “Katika mojawapo ya pembe hizo nne, paliota upembe mwingine mdogo, ukakua sana kuelekea upande wa kusini-mashariki, na kuelekea nchi ile nzuri mno.

10. Upembe huo ulikua sana kufikia viumbe vya mbinguni; ukaziangusha chini baadhi ya nyota na kuzikanyagakanyaga.

11. Upembe huo ukajikweza juu ya mkuu wa viumbe vya mbinguni. Ukakomesha tambiko za kuteketezwa ambazo mkuu wa viumbe vya mbinguni alitambikiwa kila siku, na kukufuru maskani yake.

12. Viumbe vya mbinguni vikatiwa nguvuni mwake pamoja na tambiko za kuteketezwa kila siku, kwa njia ya upotovu. Nao ukweli ukatupwa chini. Upembe huo ukaibwaga chini ibada ya kweli. Ulifanikiwa katika kila jambo ulilofanya.

13. “Kisha, nikamsikia mtakatifu mmoja akizungumza na mwenzake. Huyo mwenzake alimwuliza, ‘Je, matukio yaliyotangazwa na maono haya yataendelea kwa muda gani? Kwa muda gani sadaka za kuteketezwa za kila siku zitabaki zimebatilishwa? Kwa muda gani upotovu wa kuangamiza kila kitu utaendelea, na mahali patakatifu pamoja na viumbe vya mbingu vitaendelea kukanyagwa?’

14. Yule mtakatifu wa kwanza akamjibu, ‘Kwa muda wa nyakati za jioni na asubuhi 2,300. Kisha maskani ya Mungu itapata tena hali yake halisi.’

15. “Mimi Danieli nilipoyaona hayo maono, na nilipokuwa nikijaribu kujua maana yake, ghafla, mmoja kama mwanaadamu akasimama mbele yangu.

16. Nikasikia sauti ya mwanaadamu kutoka katika mto Ulai ikiita, ‘Gabrieli, mweleze mtu huyu maana ya maono aliyoona.’

17. Gabrieli akaja karibu na mahali niliposimama. Mimi nikaogopa sana, hata nikaanguka kifudifudi. Lakini akaniambia, ‘Wewe mtu, elewa kwamba maono uliyoyaona yanahusu wakati wa mwisho.’

18. “Alipokuwa anazungumza nami, mimi nikashikwa na usingizi mzito huku nimelala kifudifudi. Lakini yeye akanishika na kunisimamisha.

19. Kisha akaniambia, ‘Sikiliza, ninakufahamisha matokeo ya ghadhabu ya Mungu yatakavyokuwa. Maono hayo yanahusu wakati wa mwisho.

20. “ ‘Yule kondoo dume uliyemwona mwenye pembe mbili, ni wafalme wa Media na Persia.

21. Yule beberu ni mfalme wa Ugiriki. Ile pembe kubwa katikati ya macho yake ni mfalme wa kwanza.

22. Ile pembe iliyovunjika na badala yake zikaota pembe nne, ina maana kwamba ufalme huo mmoja utagawanyika kuwa falme nne, lakini falme hizo hazitakuwa na nguvu kama ule ufalme wa kwanza.

23. Wakati falme hizo zitakapofikia kikomo chake na uovu wao kufikia kilele chake, patatokea mfalme mmoja shupavu na mwerevu.

24. Atakuwa mwenye mamlaka makubwa, atasababisha uharibifu mbaya sana, na atafanikiwa katika kila atendalo. Atawaangamiza watu maarufu na watakatifu wa Mungu.

25. Kwa ujanja wake, atafanikiwa katika mipango yake ya hila, naye atajikweza. Atawaangamiza watu wengi bila taarifa, na atataka kupigana na Mkuu wa wakuu, lakini ataangamizwa pasipo kutumia nguvu za kibinadamu.

26. Maono ya hizo nyakati za jioni na za asubuhi ambayo yameelezwa ni ya kweli. Lakini uyafiche, kwani ni siri, na bado utapita muda mrefu kabla hayajatimia.’

Kusoma sura kamili Danieli 8