Agano la Kale

Agano Jipya

2 Samueli 22:1-11 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Daudi alimwimbia Mwenyezi-Mungu maneno ya wimbo ufuatao siku ile Mwenyezi-Mungu alipomkomboa mikononi mwa adui zake, na mkononi mwa Shauli.

2. Alisema,“Mwenyezi-Mungu ni mwamba wangu,ngome yangu, na mkombozi wangu.

3. Mungu wangu, mwamba wangu, ninayemkimbilia usalama;ngao yangu, nguvu ya wokovu wangu,ngome yangu na kimbilio langu.Mwokozi wangu; unaniokoa kutoka kwa watu wakatili.

4. Namwita Mwenyezi-Mungu astahiliye sifa anisaidie,nami naokolewa kutoka kwa adui zangu.

5. “Maana mawimbi ya kifo yalinizingira,mafuriko ya maangamizi yalinivamia;

6. kamba za kuzimu zilinizinga,mitego ya kifo ilinikabili.

7. “Katika taabu yangu, nilimwita Mwenyezi-Mungu;nilimwita Mungu wangu.Toka hekaluni mwake aliisikia sauti yangu,kilio changu kilimfikia masikioni mwake.

8. “Hapo, dunia ikatetemeka na kutikisika,misingi ya mbinguni ikayumbayumba na kuruka,kwani Mungu alikuwa amekasirika.

9. Moshi ulifuka kutoka puani mwake,moto uunguzao ukatoka kinywani mwake,makaa ya moto yalilipuka kutoka kwake.

10. Aliinamisha anga, akashuka chini;na wingu jeusi chini ya miguu yake.

11. Alipanda kiumbe chenye mabawa na kuruka,alionekana juu ya mabawa ya upepo.

Kusoma sura kamili 2 Samueli 22