Sura

  1. 1
  2. 2
  3. 3
  4. 4
  5. 5
  6. 6
  7. 7
  8. 8
  9. 9
  10. 10
  11. 11
  12. 12
  13. 13
  14. 14
  15. 15
  16. 16
  17. 17
  18. 18
  19. 19
  20. 20
  21. 21
  22. 22
  23. 23
  24. 24

Agano la Kale

Agano Jipya

2 Samueli 22 Biblia Habari Njema (BHN)

Wimbo wa ushindi wa Daudi

1. Daudi alimwimbia Mwenyezi-Mungu maneno ya wimbo ufuatao siku ile Mwenyezi-Mungu alipomkomboa mikononi mwa adui zake, na mkononi mwa Shauli.

2. Alisema,“Mwenyezi-Mungu ni mwamba wangu,ngome yangu, na mkombozi wangu.

3. Mungu wangu, mwamba wangu, ninayemkimbilia usalama;ngao yangu, nguvu ya wokovu wangu,ngome yangu na kimbilio langu.Mwokozi wangu; unaniokoa kutoka kwa watu wakatili.

4. Namwita Mwenyezi-Mungu astahiliye sifa anisaidie,nami naokolewa kutoka kwa adui zangu.

5. “Maana mawimbi ya kifo yalinizingira,mafuriko ya maangamizi yalinivamia;

6. kamba za kuzimu zilinizinga,mitego ya kifo ilinikabili.

7. “Katika taabu yangu, nilimwita Mwenyezi-Mungu;nilimwita Mungu wangu.Toka hekaluni mwake aliisikia sauti yangu,kilio changu kilimfikia masikioni mwake.

8. “Hapo, dunia ikatetemeka na kutikisika,misingi ya mbinguni ikayumbayumba na kuruka,kwani Mungu alikuwa amekasirika.

9. Moshi ulifuka kutoka puani mwake,moto uunguzao ukatoka kinywani mwake,makaa ya moto yalilipuka kutoka kwake.

10. Aliinamisha anga, akashuka chini;na wingu jeusi chini ya miguu yake.

11. Alipanda kiumbe chenye mabawa na kuruka,alionekana juu ya mabawa ya upepo.

12. Alijizungushia giza pande zote,kifuniko chake kilikuwa mawingu mazito na mkusanyiko wa maji.

13. Umeme ulimulika mbele yake,kulilipuka makaa ya moto.

14. Mwenyezi-Mungu alinguruma kutoka mbinguni,Mungu Mkuu akatoa sauti yake.

15. Aliwalenga adui mishale, akawatawanya,alirusha umeme, akawatimua.

16. Mwenyezi-Mungu alipowakemea,kutokana na pumzi ya puani mwake,vilindi vya bahari vilifunuliwa,misingi ya dunia ikaonekana.

17. “Mungu alinyosha mkono wake toka juu, akanichukua,kutoka kwenye maji mengi alininyanyua.

18. Aliniokoa kutoka kwa adui yangu mwenye nguvu,aliniokoa kutoka kwa hao walionichukiamaana walikuwa na nguvu nyingi kunishinda.

19. Walinivamia nilipokuwa taabuni,lakini Mwenyezi-Mungu alikuwa kinga yangu.

20. Alinileta, akaniweka mahali pa usalama,alinisalimisha, kwani alipendezwa nami.

21. “Mwenyezi-Mungu alinipa tuzo kadiri ya uadilifu wangu;alinituza kwa vile mikono yangu haina hatia.

22. Maana, nimefuata njia za Mwenyezi-Mungu,wala sikujitenga na Mungu wangu kwa uovu.

23. Nimeshika maagizo yake yote,sikuacha kufuata masharti yake.

24. Mbele yake sikuwa na hatia,nimejikinga nisiwe na hatia.

25. Mwenyezi-Mungu amenituza kadiri ya uadilifu wangu,yeye anajua usafi wangu.

26. “Wewe ni mwaminifu kwa walio waaminifu,mwema kwa wale walio wema.

27. Wewe ni mkamilifu kwa walio wakamilifu,lakini mkatili kwa watu walio waovu.

28. Wewe wawaokoa walio wanyenyekevu,lakini wawaangalia wenye majivuno kuwaporomosha.

29. Ee Mwenyezi-Mungu, wewe u taa yangu,Mungu wangu, unayefukuza giza langu.

30. Kwa msaada wako, wakishambulia kikosi;wewe wanipa nguvu ya kuruka kuta zake.

31. Anachofanya Mungu hakina dosari!Ahadi ya Mwenyezi-Mungu ni ya kuaminika;yeye ni ngao kwa wote wanaomkimbilia.

32. “Nani aliye Mungu isipokuwa Mwenyezi-Mungu?Nani aliye mwamba wa usalama ila Mungu wetu?

33. Mungu huyu ndiye kimbilio langu imara,na ameifanya njia yangu iwe salama.

34. Ameiimarisha miguu yangu kama ya paa,na kuniweka salama juu ya vilele.

35. Hunifunza kupigana vita,mikono yangu iweze kuvuta upinde wa shaba.

36. Umenipa ngao yako ya kuniokoa;msaada wako umenifanya mkuu.

37. Umenirahisishia njia yangu;wala miguu yangu haikuteleza.

38. Niliwafuatia adui zangu na kuwaangamiza,sikurudi nyuma mpaka wameangamizwa.

39. Niliwaangamiza, nikawaangusha chiniwasiweze kuinuka tena;walianguka chini ya miguu yangu.

40. Wewe ulinijalia nguvu ya kupigana vita;uliwaporomosha adui chini yangu.

41. Uliwafanya adui zangu wakimbie,na wale walionichukia niliwaangamiza.

42. Walitafuta msaada, lakini hapakuwa na wa kuwaokoa,walimlilia Mwenyezi-Mungu, lakini hakuwajibu.

43. Niliwatwanga na kuwaponda kama mavumbi ya nchi,nikawaponda na kuwakanyaga kama matope barabarani.

44. “Wewe uliniokoa na mashambulizi ya watu wangu,umenifanya mtawala wa mataifa.Watu nisiowajua walinitumikia.

45. Wageni walinijia wakinyenyekea,mara waliposikia habari zangu walinitii.

46. Wageni walikufa moyo;wakaja kutoka ngome zao wakitetemeka.

47. “Mwenyezi-Mungu yu hai!Asifiwe mwamba wangu!Atukuzwe Mungu wangu, mwamba wa wokovu wangu.

48. Yeye ameniwezesha kulipiza kisasina kuyatiisha mataifa chini yangu.

49. Ameniokoa kutoka adui zangu.Ee Mwenyezi-Mungu, ulinikuza juu ya wapinzani wanguna kunisalimisha mbali na watu wakatili.

50. “Kwa hiyo, nitakutukuza kati ya mataifa,ee Mwenyezi-Mungu, nitaliimbia sifa jina lako.

51. Mungu humjalia mfalme wake ushindi mkubwa;humwonesha fadhili zake huyo aliyemweka wakfu,naam, humfadhili Daudi na wazawa wake milele.”