Agano la Kale

Agano Jipya

2 Mambo Ya Nyakati 7:10-22 Biblia Habari Njema (BHN)

10. Siku iliyofuata ambayo ilikuwa siku ya ishirini na tatu ya mwezi wa saba, Solomoni aliwaaga watu waende kwao, wakishangilia na kufurahi moyoni kwa sababu ya wema ambao Mwenyezi-Mungu aliowajalia Daudi, Solomoni na watu wake Israeli.

11. Basi, mfalme Solomoni alimaliza kuijenga nyumba ya Mwenyezi-Mungu na ikulu na alifaulu kuyatekeleza yale yote aliyokusudia kuifanyia nyumba ya Mwenyezi-Mungu na ikulu.

12. Kisha Mwenyezi-Mungu alimtokea usiku, akamwambia, “Nimesikia sala yako na nimepachagua mahali hapa pawe nyumba yangu ya kunitolea tambiko.

13. Nikiwanyima mvua ama nikiwaletea nzige wale mimea yao au wakipatwa na maradhi mabaya

14. kama watu hao wangu wakijinyenyekesha, wakasali, wakanitafuta na kuacha njia zao mbaya, basi, mimi nitawasikiliza kutoka juu mbinguni; nitawasamehe dhambi yao na kuistawisha nchi yao.

15. Sasa nitalichunga hekalu hili na kusikiliza maombi yatakayofanyika hapa,

16. kwa maana nimeitakasa nyumba hii ili watu waliabudu jina langu hapa milele. Nitailinda na kuipenda daima.

17. Nawe, kama ukinitumikia kwa uaminifu kama Daudi baba yako alivyofanya, ukitenda yote niliyokuamuru na kutii maongozi yangu na maagizo yangu,

18. basi, mimi nitakiimarisha kiti chako cha ufalme kama nilivyofanya agano na Daudi baba yako nikisema, ‘Hutakosa mtu wa kutawala Israeli.’

19. Lakini mkiacha kunifuata, mkayaasi maongozi yangu na amri nilizowapa, na kwenda kutumikia miungu mingine na kuiabudu,

20. kwa sababu hiyo mimi nitawangoeni kutoka nchi hii ambayo nimewapa. Kadhalika na nyumba hii ambayo nimeiweka wakfu kwa ajili ya jina langu nitaitupilia mbali nami, na kuifanya kitu cha kupuuzwa na kudharauliwa miongoni mwa mataifa yote.

21. Na juu ya nyumba hii ambayo nimetukuka, kila apitaye karibu atashtuka na kuuliza, ‘Kwa nini Mwenyezi-Mungu amefanya hivyo kwa nchi hii na kwa nyumba hii?’

22. Watu wengine watajibu, ‘Ni kwa sababu walimwacha Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zao aliyewatoa nchini Misri; wakashikamana na miungu mingine, wakaiabudu na kuitumikia. Kwa hiyo Mwenyezi-Mungu amewaletea maafa haya yote.’”

Kusoma sura kamili 2 Mambo Ya Nyakati 7