Agano la Kale

Agano Jipya

1 Wafalme 20:37-43 Biblia Habari Njema (BHN)

37. Kisha, huyo mwanafunzi akamkuta mtu mwingine, akamwambia, “Nipige tafadhali.” Mtu huyo akampiga na kumjeruhi.

38. Basi, nabii akaondoka, akaenda akakaa kando ya njia, kumngojea mfalme wa Israeli, huku amejifunga kitambaa usoni, asitambulike.

39. Mfalme alipokuwa anapita, nabii akamlilia akisema, “Bwana, mimi mtumishi wako nilikuwa mstari wa mbele vitani; akaja askari mmoja, akaniletea mateka mmoja na kuniambia, ‘Mlinde mtu huyu; akitoroka utalipa kwa maisha yako wewe binafsi, au kwa vipande 3,000 vya fedha.’

40. Lakini nilipokuwa nikishughulikashughulika, mtu huyo akatoroka.” Mfalme wa Israeli akamwambia, “Ndivyo itakavyokuwa hukumu yako; umejihukumu mwenyewe.”

41. Hapo, nabii akaondoa harakaharaka kitambaa usoni mwake, naye mfalme akamtambua kuwa mmoja wa manabii.

42. Basi, nabii akamwambia mfalme, “Mwenyezi-Mungu asema hivi: ‘Kwa kuwa umemwachilia mtu ambaye niliamuru auawe akuponyoke, basi, maisha yake utalipa kwa maisha yako, na watu wake kwa watu wako.’”

43. Basi, mfalme wa Israeli akaenda zake nyumbani Samaria, amejaa chuki na huzuni nyingi.

Kusoma sura kamili 1 Wafalme 20