Agano la Kale

Agano Jipya

1 Samueli 15:13-26 Biblia Habari Njema (BHN)

13. Samueli alipomfikia Shauli, Shauli akamwambia Samueli, “Mwenyezi-Mungu na akubariki! Nimetekeleza amri ya Mwenyezi-Mungu.”

14. Samueli akamwambia, “Mbona nasikia mlio wa kondoo na ng'ombe?”

15. Shauli akajibu, “Watu waliwaacha hai kondoo na ng'ombe bora kabisa ili kumtambikia Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, lakini wengine wote tumewaangamiza.”

16. Samueli akamkatiza Shauli, “Nyamaza! Nitakuambia jambo aliloniambia Mwenyezi-Mungu leo usiku.” Shauli akasema, “Niambie.”

17. Samueli akamwambia, “Ingawa unajiona kuwa wewe si maarufu, je, wewe si kiongozi wa makabila ya Israeli? Mwenyezi-Mungu alikupaka mafuta uwe mfalme juu ya Israeli.

18. Mwenyezi-Mungu alipokutuma alikuambia, ‘Nenda ukawaangamize kabisa wale Waamaleki wenye dhambi, upigane nao hadi umewaua wote!’

19. Kwa nini basi, hukuitii sauti ya Mwenyezi-Mungu? Kwa nini mkakimbilia nyara na hivyo kutenda jambo ovu mbele ya Mwenyezi-Mungu?”

20. Shauli akajibu, “Nimetii sauti ya Mwenyezi-Mungu. Nilikwenda kule alikonituma Mwenyezi-Mungu; nimemleta Agagi mfalme wa Waamaleki, na nimewaangamiza kabisa Waamaleki.

21. Lakini watu walichukua nyara: Kondoo, ng'ombe na vitu vyote bora vilivyotolewa viangamizwe ili kumtambikia Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, huko Gilgali.”

22. Ndipo Samueli akamwambia,“Je, Mwenyezi-Mungu anapendelea zaididhabihu za kuteketezwa na matambiko,kuliko kuitii sauti yake?Tazama, kumtii yeye ni bora kuliko matambikona kumsikiliza kuliko kumtambikia mafuta ya beberu.

23. Uasi ni sawa na dhambi ya kupiga ramli,na kiburi ni sawa na uovu na kuabudu vinyago.Kwa sababu umeikataa amri ya Mwenyezi-Mungu,naye amekukataa kuwa mfalme.”

24. Shauli akamwambia Samueli, “Nimetenda dhambi. Nimeasi amri ya Mwenyezi-Mungu na amri yako, kwa sababu niliwaogopa watu, nikawatii wao.

25. Lakini sasa nakuomba, unisamehe dhambi yangu. Niruhusu nirudi pamoja nawe ili niweze kumwabudu Mwenyezi-Mungu.”

26. Samueli akamjibu: “Kamwe, siwezi kurudi pamoja nawe. Wewe umeikataa amri ya Mwenyezi-Mungu, naye amekukataa kuwa mfalme juu ya Israeli.”

Kusoma sura kamili 1 Samueli 15