Agano la Kale

Agano Jipya

Yohane 3:3-17 Biblia Habari Njema (BHN)

3. Yesu akamwambia, “Kweli nakuambia, mtu asipozaliwa tena hataweza kuuona ufalme wa Mungu.”

4. Nikodemo akamwuliza, “Mtu mzima awezaje kuzaliwa tena? Hawezi kuingia tumboni mwa mama yake na kuzaliwa tena!”

5. Yesu akamjibu, “Kweli nakuambia, mtu asipozaliwa kwa maji na Roho, hawezi kamwe kuingia katika ufalme wa Mungu.

6. Mtu huzaliwa kimwili kwa baba na mama, lakini huzaliwa kiroho kwa Roho.

7. Usistaajabu kwamba nimekuambia kuwa ni lazima kuzaliwa upya.

8. Upepo huvuma kuelekea upendako; waisikia sauti yake, lakini hujui unakotoka wala unakokwenda. Ndivyo ilivyo kwa mtu aliyezaliwa kwa Roho.”

9. Nikodemo akamwuliza, “Mambo haya yanawezekanaje?”

10. Yesu akamjibu, “Je, wewe ni mwalimu katika Israeli na huyajui mambo haya?

11. Kweli nakuambia, sisi twasema tunayoyajua na kushuhudia tuliyoyaona, lakini nyinyi hamkubali ujumbe wetu.

12. Ikiwa nimewaambieni mambo ya kidunia nanyi hamniamini, mtawezaje kuamini nikiwaambieni mambo ya mbinguni?

13. Hakuna mtu aliyepata kwenda juu mbinguni isipokuwa Mwana wa Mtu, ambaye ameshuka kutoka mbinguni.

14. “Kama vile Mose alivyomwinua juu nyoka wa shaba kule jangwani, naye Mwana wa Mtu atainuliwa juu vivyo hivyo,

15. ili kila anayemwamini awe na uhai wa milele.

16. Maana Mungu aliupenda ulimwengu hivi hata akamtoa Mwana wake wa pekee, ili kila amwaminiye asipotee, bali awe na uhai wa milele.

17. Maana Mungu hakumtuma Mwanae ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali aukomboe.

Kusoma sura kamili Yohane 3