Sura

  1. 1
  2. 2
  3. 3
  4. 4
  5. 5
  6. 6
  7. 7
  8. 8
  9. 9
  10. 10
  11. 11
  12. 12
  13. 13
  14. 14
  15. 15
  16. 16
  17. 17
  18. 18
  19. 19
  20. 20
  21. 21

Agano la Kale

Agano Jipya

Yohane 3 Biblia Habari Njema (BHN)

Yesu na Nikodemo

1. Kulikuwa na kiongozi mmoja Myahudi, wa kikundi cha Mafarisayo, jina lake Nikodemo.

2. Siku moja Nikodemo alimwendea Yesu usiku, akamwambia, “Rabi, tunajua kwamba wewe ni mwalimu uliyetumwa na Mungu, maana hakuna mtu awezaye kufanya ishara unazozifanya Mungu asipokuwa pamoja naye.”

3. Yesu akamwambia, “Kweli nakuambia, mtu asipozaliwa tena hataweza kuuona ufalme wa Mungu.”

4. Nikodemo akamwuliza, “Mtu mzima awezaje kuzaliwa tena? Hawezi kuingia tumboni mwa mama yake na kuzaliwa tena!”

5. Yesu akamjibu, “Kweli nakuambia, mtu asipozaliwa kwa maji na Roho, hawezi kamwe kuingia katika ufalme wa Mungu.

6. Mtu huzaliwa kimwili kwa baba na mama, lakini huzaliwa kiroho kwa Roho.

7. Usistaajabu kwamba nimekuambia kuwa ni lazima kuzaliwa upya.

8. Upepo huvuma kuelekea upendako; waisikia sauti yake, lakini hujui unakotoka wala unakokwenda. Ndivyo ilivyo kwa mtu aliyezaliwa kwa Roho.”

9. Nikodemo akamwuliza, “Mambo haya yanawezekanaje?”

10. Yesu akamjibu, “Je, wewe ni mwalimu katika Israeli na huyajui mambo haya?

11. Kweli nakuambia, sisi twasema tunayoyajua na kushuhudia tuliyoyaona, lakini nyinyi hamkubali ujumbe wetu.

12. Ikiwa nimewaambieni mambo ya kidunia nanyi hamniamini, mtawezaje kuamini nikiwaambieni mambo ya mbinguni?

13. Hakuna mtu aliyepata kwenda juu mbinguni isipokuwa Mwana wa Mtu, ambaye ameshuka kutoka mbinguni.

14. “Kama vile Mose alivyomwinua juu nyoka wa shaba kule jangwani, naye Mwana wa Mtu atainuliwa juu vivyo hivyo,

15. ili kila anayemwamini awe na uhai wa milele.

16. Maana Mungu aliupenda ulimwengu hivi hata akamtoa Mwana wake wa pekee, ili kila amwaminiye asipotee, bali awe na uhai wa milele.

17. Maana Mungu hakumtuma Mwanae ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali aukomboe.

18. “Anayemwamini Mwana hahukumiwi; asiyemwamini amekwisha hukumiwa, kwa sababu hakumwamini Mwana wa pekee wa Mungu.

19. Na hukumu yenyewe ndiyo hii: Mwanga umekuja ulimwenguni lakini watu wakapenda giza kuliko mwanga, kwani matendo yao ni maovu.

20. Kila mtu atendaye maovu anauchukia mwanga, wala haji kwenye mwanga, maana hapendi matendo yake maovu yamulikwe.

21. Lakini mwenye kuuzingatia ukweli huja kwenye mwanga, ili matendo yake yaonekane yametendwa kwa kumtii Mungu.”

Yesu na Yohane Mbatizaji

22. Baada ya hayo, Yesu alifika mkoani Yudea pamoja na wanafunzi wake. Alikaa huko pamoja nao kwa muda, akibatiza watu.

23. Yohane pia alikuwa akibatiza watu huko Ainoni, karibu na Salemu, maana huko kulikuwa na maji mengi. Watu walimwendea, naye akawabatiza.

24. (Wakati huo Yohane alikuwa bado hajafungwa gerezani.)

25. Ubishi ulitokea kati ya baadhi ya wanafunzi wa Yohane na Myahudi mmoja kuhusu desturi za kutawadha.

26. Basi, wanafunzi hao wakamwendea Yohane na kumwambia, “Mwalimu, yule mtu aliyekuwa pamoja nawe ngambo ya Yordani na ambaye wewe ulimshuhudia, sasa naye anabatiza, na watu wote wanamwendea.”

27. Yohane akawaambia, “Mtu hawezi kuwa na kitu asipopewa na Mungu.

28. Nanyi wenyewe mwaweza kushuhudia kuwa nilisema: ‘Mimi siye Kristo, lakini nimetumwa ili nimtangulie!’

29. Bibi arusi ni wake bwana arusi, lakini rafiki yake bwana arusi, anayesimama na kusikiliza, hufurahi sana anapomsikia bwana arusi akisema. Ndivyo furaha yangu ilivyokamilishwa.

30. Ni lazima yeye azidi kuwa maarufu, na mimi nipungue.”

Anayekuja kutoka mbinguni

31. Anayekuja kutoka juu ni mkuu kuliko wote; atokaye duniani ni wa dunia, na huongea mambo ya kidunia. Lakini anayekuja kutoka mbinguni ni mkuu kuliko wote.

32. Yeye husema yale aliyoyaona na kuyasikia, lakini hakuna mtu anayekubali ujumbe wake.

33. Lakini mtu yeyote anayekubali ujumbe wake anathibitisha kwamba Mungu ni kweli.

34. Yule aliyetumwa na Mungu husema maneno ya Mungu, maana Mungu humjalia mtu huyo Roho wake bila kipimo.

35. Baba anampenda Mwana na amemkabidhi vitu vyote.

36. Anayemwamini Mwana anao uhai wa milele; asiyemwamini Mwana hatakuwa na uhai wa milele, bali ghadhabu ya Mungu hubaki juu yake.