Sura

  1. 1
  2. 2
  3. 3
  4. 4
  5. 5
  6. 6
  7. 7
  8. 8
  9. 9
  10. 10
  11. 11
  12. 12
  13. 13
  14. 14
  15. 15
  16. 16
  17. 17
  18. 18
  19. 19
  20. 20
  21. 21

Agano la Kale

Agano Jipya

Yohane 2 Biblia Habari Njema (BHN)

Harusi mjini Kana

1. Siku ya tatu kulikuwa na harusi mjini Kana, mkoani Galilaya. Mama yake Yesu alikuwapo,

2. naye Yesu alikuwa amealikwa harusini pamoja na wanafunzi wake.

3. Divai ilipokwisha, mama yake akamwambia, “Hawana divai!”

4. Yesu akamjibu, “Mama, usiniambie la kufanya. Saa yangu bado.”

5. Hapo mama yake akawaambia watumishi, “Lolote atakalowaambieni, fanyeni.”

6. Hapo palikuwa na mitungi sita ya mawe, ambayo kila mmoja uliweza kuchukua kiasi cha madebe mawili au matatu. Ilikuwa imewekwa hapo kufuatana na desturi ya Kiyahudi ya kutawadha.

7. Yesu akawaambia, “Ijazeni mitungi hiyo maji.” Nao wakaijaza mpaka juu.

8. Kisha akawaambia, “Sasa choteni mkampelekee mkuu wa karamu.”

9. Mkuu wa karamu alipoonja hayo maji, kumbe yalikuwa yamegeuka kuwa divai. Yeye hakujua ilikotoka, (lakini wale watumishi waliochota maji walijua). Mkuu wa karamu akamwita bwana arusi,

10. akamwambia, “Kila mtu huandaa divai nzuri kwanza hata wakisha tosheka huandaa ile hafifu. Lakini wewe umeiweka divai nzuri mpaka sasa!”

11. Yesu alifanya ishara hii ya kwanza huko Kana, Galilaya, akaonesha utukufu wake; nao wanafunzi wake wakamwamini.

12. Baada ya hayo, Yesu alishuka pamoja na mama yake, ndugu zake na wanafunzi wake, wakaenda Kafarnaumu ambako walikaa kwa siku chache.

Yesu hekaluni

13. Sikukuu ya Wayahudi ya Pasaka ilikuwa imekaribia; hivyo Yesu akaenda juu Yerusalemu.

14. Basi, akawakuta mle hekaluni watu wakiuza ng'ombe, kondoo na njiwa, na wavunja fedha walikuwa wamekaa kwenye meza zao.

15. Akatengeneza mjeledi wa kamba, akawafukuza wote nje ya hekalu pamoja na kondoo na ng'ombe wao, akazitawanya sarafu za wenye kuvunja fedha na kupindua meza zao.

16. Akawaambia wale waliokuwa wanauza njiwa, “Ondoeni vitu hivi hapa. Msiifanye nyumba ya Baba yangu kuwa soko!”

17. Wanafunzi wake wakakumbuka kwamba Maandiko yasema: “Upendo wangu kwa nyumba yako waniua.”

18. Baadhi ya Wayahudi wakamwuliza Yesu, “Utafanya mwujiza gani kuonesha kwamba unayo haki kufanya mambo haya?”

19. Yesu akawaambia, “Vunjeni hekalu hili, nami nitalijenga kwa siku tatu.”

20. Hapo Wayahudi wakasema, “Hekalu hili lilijengwa kwa muda wa miaka arubaini na sita. Je, wewe utalijenga kwa siku tatu?”

21. Lakini Yesu alikuwa anaongea juu ya hekalu ambalo ni mwili wake.

22. Basi, alipofufuliwa kutoka kwa wafu, wanafunzi wake walikumbuka kwamba alikuwa amesema hayo, wakayaamini Maandiko Matakatifu na yale maneno ambayo Yesu alikuwa amesema.

Yesu ajua mioyo ya watu wote

23. Yesu alipokuwa Yerusalemu kwa sikukuu ya Pasaka, watu wengi walimwamini walipoona ishara alizofanya.

24. Lakini Yesu hakuwa na imani nao kwa sababu aliwajua wote.

25. Hakuhitaji kuambiwa chochote juu ya watu, maana aliyajua barabara mambo yote yaliyomo mioyoni mwao.