Agano la Kale

Agano Jipya

Wakolosai 3:11-23 Biblia Habari Njema (BHN)

11. Katika hali hii, hakuna tena tofauti kati ya Mgiriki na Myahudi, aliyetahiriwa na asiyetahiriwa, msomi na asiye msomi, mtumwa na mtu aliye huru. Kristo ni kila kitu, na yumo katika yote.

12. Nyinyi ni watu wake Mungu; yeye aliwapenda na kuwateua. Kwa hiyo, basi, vaeni moyo wa huruma, wema, unyenyekevu, upole na uvumilivu.

13. Vumilianeni na kusameheana iwapo mmoja wenu analo jambo lolote dhidi ya mwenzake. Mnapaswa kusameheana kama Bwana alivyowasamehe nyinyi.

14. Zaidi ya hayo yote, zingatieni upendo, kwani upendo huunganisha kila kitu katika umoja ulio kamili.

15. Nayo amani ya Kristo itawale mioyoni mwenu; maana kwa ajili hiyo nyinyi mmeitwa katika mwili huo mmoja. Tena muwe na shukrani!

16. Ujumbe wa Kristo na ukae ndani yenu pamoja na utajiri wake wote. Fundishaneni na kushauriana kwa hekima yote. Imbeni Zaburi, nyimbo na tenzi za kiroho; mwimbieni Mungu mioyoni mwenu kwa shukrani.

17. Na, kila mfanyacho kwa neno au tendo, fanyeni vyote kwa jina la Bwana Yesu na kumshukuru Mungu Baba kwa njia yake.

18. Enyi wake, watiini waume zenu, kwani ndivyo apendavyo Bwana.

19. Nanyi waume, wapendeni wake zenu, na msiwe wakali kwao.

20. Enyi watoto, watiini wazazi wenu daima maana hiyo humpendeza Bwana.

21. Nanyi wazazi, msiwachukize watoto wenu, la sivyo watakata tamaa.

22. Enyi watumwa, watiini wakuu wenu wa kidunia katika mambo yote, na si tu wakati wanapowatazama kwa kuwa mnataka kujipendekeza kwao; ila fanyeni hivyo kwa moyo wote, kwa sababu ya kumcha Bwana.

23. Kila mfanyacho, fanyeni kwa moyo wote, kwa sababu ya Bwana na si kwa ajili ya mtu.

Kusoma sura kamili Wakolosai 3