Sura

  1. 1
  2. 2
  3. 3
  4. 4
  5. 5
  6. 6
  7. 7
  8. 8
  9. 9
  10. 10
  11. 11
  12. 12
  13. 13
  14. 14
  15. 15
  16. 16
  17. 17
  18. 18
  19. 19
  20. 20
  21. 21
  22. 22
  23. 23
  24. 24
  25. 25
  26. 26
  27. 27
  28. 28

Agano la Kale

Agano Jipya

Mathayo 15 Biblia Habari Njema (BHN)

Mapokeo ya mababu

1. Kisha Mafarisayo na waalimu wa sheria wakafika kutoka Yerusalemu, wakamwendea Yesu, wakamwuliza,

2. “Kwa nini wanafunzi wako hawajali mapokeo tuliyopokea kwa wazee wetu? Hawanawi mikono ipasavyo kabla ya kula!”

3. Yesu akawajibu, “Kwa nini nanyi hamjali sheria ya Mungu ila mnapendelea mapokeo yenu wenyewe?

4. Mungu amesema: ‘Waheshimu baba yako na mama yako,’ na ‘Anayemtukana baba yake au mama yake, lazima auawe.’

5. Lakini nyinyi mwafundisha ati mtu akiwa na kitu ambacho angeweza kumsaidia nacho baba yake au mama yake, lakini akasema: ‘Kitu hiki nimemtolea Mungu,’

6. basi, hapaswi tena kumheshimu baba yake! Ndivyo mnavyodharau neno la Mungu kwa kufuata mafundisho yenu wenyewe.

7. Enyi wanafiki! Isaya alitabiri sawa kabisa juu yenu:

8. ‘Mungu asema: Watu hawa huniheshimu kwa maneno tu,lakini mioyoni mwao wako mbali nami.

9. Kuniabudu kwao hakufai,maana mambo wanayofundisha ni maagizo ya kibinadamu tu.’”

Mambo yanayomtia mtu unajisi

10. Yesu aliuita ule umati wa watu, akawaambia, “Sikilizeni, mkaelewe!

11. Kitu kinachomtia mtu unajisi si kile kiingiacho kinywani, bali kile kitokacho kinywani. Hicho ndicho kimtiacho mtu unajisi.”

12. Kisha wanafunzi wakamwendea, wakamwambia, “Je, unajua kwamba Mafarisayo walichukizwa waliposikia maneno yako?”

13. Lakini yeye akawajibu, “Kila mmea ambao Baba yangu aliye mbinguni hakupanda, utangolewa.

14. Waacheni wenyewe! Wao ni vipofu, viongozi wa vipofu; na kipofu akimwongoza kipofu, wote wawili hutumbukia shimoni.”

15. Petro akasema, “Tufafanulie huo mfano.”

16. Yesu akasema, “Hata nyinyi hamwelewi?

17. Je, hamwelewi kwamba kila kinachoingia kinywani huenda tumboni na baadaye hutolewa nje chooni?

18. Lakini mambo yatokayo kinywani hutoka moyoni, na hayo ndiyo yanayomtia mtu unajisi.

19. Maana moyoni hutoka mawazo ya uuaji, uzinzi, uasherati, wizi, ushahidi wa uongo na kashfa.

20. Hayo ndiyo yanayomtia mtu unajisi. Lakini kula chakula bila kunawa mikono hakumtii mtu unajisi.”

Imani ya mama mmoja

21. Yesu aliondoka mahali hapo akaenda kukaa katika sehemu za Tiro na Sidoni.

22. Basi, mama mmoja Mkanaani wa nchi hiyo alimjia, akapaza sauti: “Bwana, Mwana wa Daudi, nionee huruma! Binti yangu anasumbuliwa na pepo.”

23. Lakini Yesu hakumjibu neno. Basi, wanafunzi wake wakamwendea, wakamwambia, “Mwambie aende zake kwa maana anatufuatafuata akipiga kelele.”

24. Yesu akajibu, “Sikutumwa ila kwa watu wa Israeli waliopotea kama kondoo.”

25. Hapo huyo mama akaja, akamsujudia, akasema, “Bwana, nisaidie.”

26. Yesu akamjibu, “Si vizuri kuchukua chakula cha watoto na kuwatupia mbwa.”

27. Huyo mama akajibu, “Ni kweli, Bwana; lakini hata mbwa hula makombo yanayoanguka kutoka meza ya bwana wao.”

28. Hapo Yesu akamjibu, “Mama, imani yako ni kubwa; basi, ufanyiwe kama unavyotaka.” Yule binti yake akapona wakati huohuo.

Yesu anawaponya watu wengi

29. Yesu alitoka hapo akaenda kando ya ziwa Galilaya, akapanda mlimani, akaketi.

30. Watu wengi sana wakamjia wakiwaleta vilema, vipofu, viwete, bubu na wengine wengi waliokuwa wagonjwa, wakawaweka mbele ya miguu yake, naye Yesu akawaponya.

31. Umati ule wa watu ulishangaa sana ulipoona bubu wakiongea, waliokuwa wamelemaa wamepona, viwete wakitembea na vipofu wakiona; watu wakamsifu Mungu wa Israeli.

Yesu anawapa chakula watu elfu nne

32. Basi, Yesu aliwaita wanafunzi wake, akasema, “Nawaonea huruma watu hawa kwa sababu wamekuwa nami kwa siku tatu, wala hawana chakula. Sipendi kuwaacha waende zao bila kula, wasije wakazimia njiani.”

33. Wanafunzi wakamwambia, “Hapa tuko nyikani; tutapata wapi chakula cha kuwatosha watu wengi hivi?”

34. Yesu akawauliza, “Mnayo mikate mingapi?” Wakamjibu, “Saba na visamaki vichache.”

35. Basi, Yesu akawaamuru watu wakae chini.

36. Akaitwaa ile mikate saba na vile visamaki, akamshukuru Mungu, akavimega, akawapa wanafunzi, nao wakawagawia watu.

37. Wote wakala, wakashiba. Kisha wakakusanya mabaki, wakajaza vikapu saba.

38. Hao waliokula walikuwa wanaume 4,000, bila kuhesabu wanawake na watoto.

39. Basi, Yesu akawaaga watu, akapanda mashua, akaenda katika eneo la Magadani.