Sura

  1. 1
  2. 2
  3. 3
  4. 4
  5. 5
  6. 6
  7. 7
  8. 8
  9. 9
  10. 10
  11. 11
  12. 12
  13. 13
  14. 14
  15. 15
  16. 16
  17. 17
  18. 18
  19. 19
  20. 20
  21. 21
  22. 22
  23. 23
  24. 24
  25. 25
  26. 26
  27. 27
  28. 28

Agano la Kale

Agano Jipya

Matendo 2 Biblia Habari Njema (BHN)

Roho Mtakatifu anawashukia waumini

1. Siku ya Pentekoste ilipofika, waumini wote walikuwa wamekusanyika mahali pamoja.

2. Ghafla, sauti ikasikika kutoka angani; sauti iliyokuwa kama ya upepo mkali, ikaijaza ile nyumba yote walimokuwa wamekaa.

3. Kisha, vikatokea vitu vilivyoonekana kama ndimi za moto, vikagawanyika na kutua juu ya kila mmoja wao.

4. Wote wakajazwa Roho Mtakatifu, wakaanza kusema lugha mbalimbali kadiri Roho alivyowawezesha.

5. Na huko Yerusalemu walikuwako Wayahudi, watu wamchao Mungu, waliotoka katika kila nchi duniani.

6. Waliposikia sauti hiyo, kundi kubwa la watu lilikusanyika. Wote walishtuka sana kwani kila mmoja wao aliwasikia hao waumini wakisema kwa lugha yake mwenyewe.

7. Walistaajabu na kushangaa wakisema, “Je, hawa wote tunaowasikia wakisema hivi, si wenyeji wa Galilaya?

8. Imekuwaje, basi, kwamba kila mmoja wetu anawasikia wakisema kwa lugha yake mwenyewe?

9. Baadhi yetu ni Waparthi, Wamedi na Waelamu; wengine ni wenyeji wa Mesopotamia, Yudea, Kapadokia, Ponto na Asia,

10. Frugia na Pamfulia, Misri na sehemu za Libia karibu na Kurene; wengine wetu ni wageni kutoka Roma,

11. Wayahudi na watu walioongokea dini ya Kiyahudi; wengine wametoka Krete na Arabia. Sisi sote tunasikia wakisema kwa lugha zetu wenyewe mambo makuu ya Mungu.”

12. Wote walishangaa na kufadhaika huku wakiulizana, “Hii ina maana gani?”

13. Lakini wengine wakawadhihaki wakisema, “Watu hawa wamelewa divai mpya!”

Hotuba ya Petro

14. Lakini Petro alisimama pamoja na wale kumi na mmoja akaanza kuwahutubia watu kwa sauti kubwa: “Ndugu Wayahudi nanyi nyote mnaokaa hapa Yerusalemu, sikilizeni kwa makini maneno yangu.

15. Watu hawa hawakulewa kama mnavyodhani; mbona ni saa tatu tu asubuhi?

16. Ukweli ni kwamba jambo hili ni lile alilosema nabii Yoeli:

17. ‘Katika siku zile za mwisho, asema Bwana,nitawamiminia binadamu wote Roho wangu.Watoto wenu wa kiume na wa kike watatoa unabii,vijana wenu wataona maono,na wazee wenu wataota ndoto.

18. Naam, hata watumishi wangu wa kiume na kike,nitawamiminia Roho wangu siku zile,nao watatoa unabii.

19. Nitatenda miujiza juu angani,na ishara chini duniani;kutakuwa na damu, moto na moshi mzito;

20. jua litatiwa giza,na mwezi utakuwa mwekundu kama damu,kabla ya kutokea ile siku kuu na tukufu ya Bwana.

21. Hapo, yeyote atakayeomba kwa jina la Bwana, ataokolewa.’

22. “Wananchi wa Israeli, sikilizeni maneno haya! Yesu wa Nazareti alikuwa mtu ambaye mamlaka yake ya kimungu yalithibitishwa kwenu kwa miujiza, maajabu na ishara Mungu alizofanya kati yenu kwa njia yake, kama mnavyojua.

23. Kufuatana na mpango wake mwenyewe Mungu alikwisha amua kwamba Yesu angetiwa mikononi mwenu; nanyi mkamuua kwa kuwaachia watu wabaya wamsulubishe.

24. Lakini Mungu alimfufua kutoka kwa wafu, akamwokoa katika maumivu ya kifo kwa maana haingewezekana kabisa kifo kimfunge.

25. Maana Daudi alisema juu yake hivi:‘Nilimwona Bwana mbele yangu daima;yuko nami upande wangu wa kulia hata sitatikisika.

26. Kwa hiyo, moyo wangu ulifurahi;tena nilipiga vigelegele vya furaha.Mwili wangu utakaa katika tumaini,

27. maana hutaiacha roho yangu kuzimu,wala kumruhusu mtakatifu wako aoze.

28. Umenionesha njia za uhai,umenijaza furaha kwa kuwako kwako!’

29. “Ndugu zangu, napenda kuwaambieni waziwazi juu ya mambo yaliyompata Daudi, babu yetu. Yeye alikufa, akazikwa, tena kaburi lake liko papa hapa petu mpaka leo.

30. Lakini kwa vile Daudi alikuwa nabii, alijua kuwa Mungu alimwapia kiapo kwamba atamtawaza mmoja wa uzawa wake kuwa mfalme mahali pake.

31. Daudi aliona kabla mambo yatakayofanywa na Mungu na hivyo akasema juu ya ufufuo wa Kristo wakati aliposema: ‘Hakuachwa kuzimu, mwili wake haukuoza.’

32. Basi, Mungu alimfufua huyo Yesu na sisi sote ni mashahidi wa tukio hilo.

33. Yesu alipokwisha pandishwa na kuwekwa na Mungu upande wake wa kulia, akapokea kutoka kwake Baba yule Roho Mtakatifu ambaye alituahidi, ametumiminia huyo Roho. Hicho ndicho mnachoona sasa na kusikia.

34. Maana Daudi mwenyewe, hakupanda mpaka mbinguni; ila yeye alisema:‘Bwana alimwambia Bwana wangu:Keti upande wangu wa kulia,

35. hadi niwafanye adui zako kiti cha miguu yako.’

36. “Watu wote wa Israeli wanapaswa kufahamu kwa hakika kwamba huyo Yesu mliyemsulubisha, ndiye huyo ambaye Mungu amemfanya kuwa Bwana na Kristo.”

37. Basi, watu waliposikia hayo, walichomwa moyo, wakawauliza Petro na wale mitume wenzake: “Ndugu zetu, tufanye nini?”

38. Petro akajibu, “Tubuni na kila mmoja wenu abatizwe kwa jina la Yesu Kristo ili mpate kuondolewa dhambi zenu na kupokea ile ahadi ya Roho Mtakatifu.

39. Maana, ahadi ile ilikuwa kwa ajili yenu, kwa ajili ya watoto wenu, kwa ajili ya wote wanaokaa mbali na kwa ajili ya kila mtu ambaye Bwana Mungu wetu atamwita kwake.”

40. Kwa maneno mengine mengi, Petro alisisitiza na kuwahimiza watu akisema, “Jiokoeni katika kizazi hiki kiovu.”

41. Wengi waliyakubali maneno yake, wakabatizwa. Watu wapatao 3,000 wakaongezeka katika kile kikundi siku hiyo.

42. Hawa wote waliendelea kujifunza kutoka kwa mitume, kuishi pamoja kindugu, kumega mkate na kusali.

Maisha ya kila siku ya wale waumini

43. Miujiza na maajabu mengi yalifanyika kwa njia ya mitume hata kila mtu akajawa na hofu.

44. Waumini wote waliendelea kuwa kitu kimoja na mali zao waligawiana.

45. Walikuwa wakiuza mali na vitu vyao kisha wakagawana fedha kadiri ya mahitaji ya kila mmoja.

46. Waliendelea kukutana pamoja kila siku hekaluni. Lakini wakati wa kumega mkate, walikutana katika nyumba zao na wakakishiriki chakula hicho kwa furaha na moyo mkunjufu.

47. Walimtukuza Mungu, wakapendwa na watu wote. Kila siku Bwana aliwaongezea idadi ya watu waliokuwa wakiokolewa.