Agano la Kale

Agano Jipya

Matendo 14:8-25 Biblia Habari Njema (BHN)

8. Kulikuwa na mtu mmoja huko Lustra ambaye alikuwa kiwete tangu kuzaliwa, na alikuwa hajapata kutembea kamwe.

9. Mtu huyo alikuwa anamsikiliza Paulo alipokuwa anahubiri. Paulo alimtazama kwa makini, na alipoona kuwa alikuwa na imani ya kuweza kuponywa,

10. akasema kwa sauti kubwa, “Simama wima kwa miguu yako!” Huyo mtu aliyelemaa miguu akainuka ghafla, akaanza kutembea.

11. Umati wa watu walipoona alichofanya Paulo, walianza kupiga kelele kwa lugha ya Kilukaonia: “Miungu imetujia katika sura za binadamu!”

12. Barnaba akaitwa Zeu, na Paulo, kwa vile yeye ndiye aliyekuwa anaongea, akaitwa Herme.

13. Naye kuhani wa hekalu la Zeu lililokuwa nje ya mji akaleta fahali na shada za maua mbele ya mlango mkuu wa mji, naye pamoja na ule umati wa watu akataka kuwatambikia mitume.

14. Barnaba na Paulo walipopata habari hizo waliyararua mavazi yao na kukimbilia katika lile kundi la watu wakisema kwa sauti kubwa:

15. “Ndugu, kwa nini mnafanya mambo hayo? Sisi pia ni binadamu kama nyinyi. Na, tuko hapa kuwahubirieni Habari Njema, mpate kuziacha hizi sanamu tupu, mkamgeukie Mungu aliye hai, Mungu aliyeumba mbingu na dunia, bahari na vyote vilivyomo.

16. Zamani Mungu aliruhusu kila taifa lifanye lilivyopenda.

17. Hata hivyo, Mungu hakuacha kujidhihirisha kwa mambo mema anayowatendea: Huwanyeshea mvua toka angani, huwapa mavuno kwa wakati wake, huwapa chakula na kuijaza mioyo yenu furaha.”

18. Ingawa walisema hivyo haikuwa rahisi kuwazuia wale watu wasiwatambikie.

19. Lakini Wayahudi kadhaa walikuja kutoka Antiokia na Ikonio, wakawafanya watu wajiunge nao, wakampiga mawe Paulo na kumburuta hadi nje ya mji wakidhani amekwisha kufa.

20. Lakini waumini walipokusanyika na kumzunguka, aliamka, akarudi mjini. Kesho yake, yeye pamoja na Barnaba walikwenda Derbe.

21. Baada ya Paulo na Barnaba kuhubiri Habari Njema huko Derbe na kupata wafuasi wengi, walifunga safari kwenda Antiokia kwa kupitia Lustra na Ikonio.

22. Waliwaimarisha waumini wa miji hiyo na kuwatia moyo wabaki imara katika imani. Wakawaambia, “Ni lazima sisi sote kupitia katika taabu nyingi ili tuingie katika ufalme wa Mungu.”

23. Waliteua wazee katika kila kanisa kwa ajili ya waumini, kisha, kwa kusali na kufunga, wakawaweka chini ya ulinzi wa Bwana ambaye walikuwa wanamwamini.

24. Baada ya kupitia katika nchi ya Pisidia, walifika Pamfulia.

25. Baada ya kuhubiri ule ujumbe huko Perga, walikwenda Atalia.

Kusoma sura kamili Matendo 14