Agano la Kale

Agano Jipya

Matendo 11:11-25 Biblia Habari Njema (BHN)

11. Ghafla, watu watatu waliokuwa wametumwa kwangu kutoka Kaisarea waliwasili kwenye nyumba nilimokuwa nakaa.

12. Roho aliniambia niende pamoja nao bila kusita. Hawa ndugu sita waliandamana nami pia kwenda Kaisarea na huko tuliingia nyumbani mwa Kornelio.

13. Yeye alitueleza jinsi alivyokuwa amemwona malaika amesimama nyumbani mwake na kumwambia: ‘Mtume mtu Yopa akamwite mtu mmoja aitwaye Simoni, kwa jina lingine Petro.

14. Yeye atakuambia maneno ambayo kwayo wewe na jamaa yako yote mtaokolewa.’

15. Na nilipoanza tu kuongea, Roho Mtakatifu aliwashukia kama alivyotushukia sisi pale awali.

16. Hapo nilikumbuka yale maneno Bwana aliyosema: ‘Yohane alibatiza kwa maji, lakini nyinyi mtabatizwa kwa Roho Mtakatifu.’

17. Basi, kama Mungu amewapa pia watu wa mataifa mengine kipawa kilekile alichotupa sisi tulipomwamini Bwana Yesu Kristo, je, mimi ni nani hata nijaribu kumpinga Mungu?”

18. Waliposikia hayo, waliacha ubishi, wakamtukuza Mungu wakisema, “Mungu amewapa watu wa mataifa mengine nafasi ya kutubu wapate uhai!”

19. Kutokana na mateso yaliyotokea wakati Stefano alipouawa, waumini walitawanyika. Wengine walikwenda mpaka Foinike, Kupro na Antiokia wakihubiri ule ujumbe kwa Wayahudi tu.

20. Lakini baadhi ya waumini waliotoka Kupro na Kurene, walikwenda Antiokia wakautangaza huo ujumbe kwa watu wa mataifa mengine wakiwahubiria Habari Njema juu ya Bwana Yesu.

21. Bwana aliwasaidia na idadi kubwa ya watu iliamini na kumgeukia Bwana.

22. Habari ya jambo hilo ikasikika kwa lile kanisa la Yerusalemu. Hivyo wakamtuma Barnaba aende Antiokia.

23. Alipofika huko na kuona jinsi Mungu alivyowaneemesha wale watu, alifurahi na kuwahimiza wote wadumu katika uaminifu wao kwa Bwana.

24. Barnaba alikuwa mtu mwema na mwenye kujaa Roho Mtakatifu na imani. Kundi kubwa la watu lilivutwa kwa Bwana.

25. Kisha, Barnaba alikwenda Tarso kumtafuta Saulo.

Kusoma sura kamili Matendo 11