Sura

  1. 1
  2. 2
  3. 3
  4. 4
  5. 5
  6. 6
  7. 7
  8. 8
  9. 9
  10. 10
  11. 11
  12. 12
  13. 13
  14. 14
  15. 15
  16. 16

Agano la Kale

Agano Jipya

Marko 3 Biblia Habari Njema (BHN)

Yesu anamponya mwenye mkono uliopooza

1. Yesu aliingia tena katika sunagogi na mle ndani mlikuwa na mtu aliyekuwa na mkono uliopooza.

2. Humo, baadhi ya watu walimngojea amponye mtu huyo siku ya Sabato ili wapate kumshtaki.

3. Yesu akamwambia huyo mtu aliyekuwa na mkono uliopooza, “Njoo hapa katikati.”

4. Kisha, akawauliza, “Je, ni halali siku ya Sabato kutenda jambo jema au kutenda jambo baya; kuokoa maisha au kuua?” Lakini wao hawakusema neno.

5. Hapo akawatazama wote kwa hasira, akaona huzuni kwa sababu ya ugumu wa mioyo yao. Kisha akamwambia yule mtu, “Nyosha mkono wako!” Naye akaunyosha mkono wake, ukawa mzima tena.

6. Mara Mafarisayo wakatoka nje, wakafanya shauri pamoja na watu wa kikundi cha Herode jinsi ya kumwangamiza Yesu.

Umati wa watu kando ya ziwa

7. Yesu aliondoka hapo pamoja na wanafunzi wake, akaenda kando ya ziwa, na umati wa watu ukamfuata. Watu hao walikuwa wametoka Yerusalemu, Yudea,

8. Idumea, ngambo ya mto Yordani, Tiro na Sidoni. Watu hao wengi walimwendea Yesu kwa sababu ya kusikia mambo mengi aliyokuwa ameyatenda.

9. Yesu akawaambia wanafunzi wake wamtayarishie mashua moja, ili umati wa watu usije ukamsonga.

10. Alikuwa amewaponya watu wengi, na wagonjwa wote wakawa wanamsonga ili wapate kumgusa.

11. Na watu waliokuwa wamepagawa na pepo wachafu walipomwona, walijitupa chini mbele yake na kupaza sauti, “Wewe ni Mwana wa Mungu!”

12. Lakini Yesu akawaamuru kwa ukali wasimjulishe kwa watu.

Yesu anawateua mitume kumi na wawili

13. Yesu alipanda kilimani, akawaita wale aliowataka. Basi, wakamwendea,

14. naye akawateua watu kumi na wawili ambao aliwaita mitume, wakae naye, awatume kuhubiri

15. na wawe na uwezo wa kuwafukuza pepo.

16. Basi, hao kumi na wawili walioteuliwa ndio hawa: Simoni (ambaye Yesu alimpa jina, Petro),

17. Yakobo na Yohane, wana wa Zebedayo (Yesu aliwapa hawa ndugu wawili jina Boanerge, maana yake “Wanangurumo”),

18. Andrea na Filipo, Bartholomayo, Mathayo, Thoma, Yakobo mwana wa Alfayo, Thadayo, Simoni Mkanaani na

19. Yuda Iskarioti ambaye alimsaliti Yesu.

Yesu na Beelzebuli

20. Kisha Yesu alikwenda nyumbani. Umati wa watu ukakusanyika tena, hata Yesu na wafuasi wake wasiweze kupata nafasi ya kula chakula.

21. Basi, watu wa jamaa yake walipopata habari hiyo wakatoka kwenda kumchukua maana walikuwa wanasema kwamba ana wazimu.

22. Nao waalimu wa sheria waliokuwa wametoka Yerusalemu, wakasema, “Ana Beelzebuli! Tena, anawafukuza pepo kwa nguvu ya mkuu wa pepo.”

23. Hapo Yesu akawaita, akawaambia kwa mifano, “Shetani anawezaje kumfukuza Shetani?

24. Ikiwa utawala mmoja umegawanyika makundimakundi yanayopingana, utawala huo hauwezi kudumu.

25. Tena, ikiwa jamaa moja imegawanyika makundimakundi yanayopingana, jamaa hiyo itaangamia.

26. Ikiwa basi, utawala wa Shetani umegawanyika vikundivikundi hauwezi kudumu, bali utaangamia kabisa.

27. “Hakuna mtu awezaye kuivamia nyumba ya mtu mwenye nguvu na kumnyanganya mali yake, isipokuwa kwanza amemfunga huyo mtu mwenye nguvu; hapo ndipo atakapoweza kumnyanganya mali yake.

28. “Kweli nawaambieni, watu watasamehewa dhambi zao zote na kufuru zao zote;

29. lakini anayesema mabaya dhidi ya Roho Mtakatifu, hatasamehewa kamwe; ana hatia ya dhambi ya milele.” (

30. Yesu alisema hivyo kwa sababu walikuwa wanasema, “Ana pepo mchafu.”)

Mama na ndugu za Yesu

31. Mama yake Yesu na ndugu zake walifika hapo, wakasimama nje, wakampelekea ujumbe kumwita.

32. Umati wa watu ulikuwa umekaa hapo kumzunguka. Basi, watu wakamwambia, “Mama yako na ndugu zako wako nje, wanataka kukuona.”

33. Yesu akawaambia, “Mama yangu na ndugu zangu ni kina nani?”

34. Hapo akawatazama watu waliokuwa wamemzunguka, akasema, “Tazameni! Hawa ndio mama yangu na ndugu zangu.

35. Mtu yeyote anayefanya anayotaka Mungu, huyo ndiye kaka yangu, dada yangu na mama yangu.”