Agano la Kale

Agano Jipya

Marko 12:9-23 Biblia Habari Njema (BHN)

9. “Basi, mwenye shamba atafanya nini? Atakuja kuwaangamiza hao wakulima na kulikodisha hilo shamba la mizabibu kwa watu wengine.

10. Je, hamjasoma Maandiko haya?‘Jiwe walilokataa waashisasa limekuwa jiwe kuu la msingi.

11. Bwana ndiye aliyefanya jambo hili,nalo ni la ajabu sana kwetu.’”

12. Makuhani wakuu, waalimu wa sheria na wazee walifahamu ya kwamba mfano huo ulikuwa unawahusu. Kwa hiyo walijaribu kumtia nguvuni, lakini waliogopa umati wa watu. Basi, wakamwacha, wakaenda zao.

13. Basi, baadhi ya Mafarisayo na wafuasi wa kikundi cha Herode walitumwa ili wamtege Yesu kwa maneno yake.

14. Wakamwendea, wakamwambia, “Mwalimu, tunajua kwamba wewe ni mtu mwaminifu unayesema ukweli mtupu, wala humjali mtu yeyote. Wala cheo cha mtu si kitu kwako, lakini wafundisha ukweli kuhusu njia ya Mungu. Je, ni halali kulipa kodi kwa Kaisari, au la? Tulipe au tusilipe?”

15. Lakini Yesu alijua unafiki wao, akawaambia, “Mbona mnanijaribu? Nionesheni hiyo sarafu.”

16. Wakamwonesha. Naye akawauliza, “Sura na chapa hii ni ya nani?” Wakamjibu, “Ni ya Kaisari.”

17. Basi, Yesu akawaambia, “Ya Kaisari mpeni Kaisari, na ya Mungu mpeni Mungu.” Wakashangazwa sana naye.

18. Masadukayo ambao husema kwamba hakuna ufufuo walimwendea Yesu, wakamwuliza,

19. “Mwalimu, Mose alituagiza hivi: ‘Mtu akifa na kuacha mke bila mtoto, ndugu yake lazima amchukue huyo mama mjane, ili ampatie ndugu yake watoto.’

20. Basi, kulikuwa na ndugu saba. Wa kwanza alioa, akafa bila kuacha mtoto.

21. Ndugu wa pili akamwoa huyo mjane, naye pia akafa bila kuacha mtoto; na ndugu watatu hali kadhalika.

22. Wote saba walikufa bila kuacha mtoto. Mwishowe yule mama mjane naye akafa.

23. Basi, siku watu watakapofufuka, mama huyo atakuwa mke wa nani? Wote saba walikuwa wamemwoa.”

Kusoma sura kamili Marko 12