Agano la Kale

Agano Jipya

Luka 13:26-35 Biblia Habari Njema (BHN)

26. Nanyi mtaanza kumwambia: ‘Sisi ndio wale tuliokula na kunywa pamoja nawe; na wewe ulifundisha katika vijiji vyetu.’

27. Lakini yeye atasema: ‘Sijui nyinyi mmetoka wapi; ondokeni mbele yangu, enyi nyote watenda maovu.’

28. Ndipo kutakuwa na kulia na kusaga meno, wakati mtakapowaona Abrahamu, Isaka na Yakobo na manabii wote wapo katika ufalme wa Mungu, lakini nyinyi wenyewe mmetupwa nje!

29. Watu watakuja kutoka mashariki na magharibi, kutoka kaskazini na kusini na kukaa kwenye karamu katika ufalme wa Mungu.

30. Naam, wale walio wa mwisho watakuwa wa kwanza; na wale walio wa kwanza watakuwa wa mwisho.”

31. Wakati huohuo, Mafarisayo na watu wengine walimwendea Yesu wakamwambia, “Ondoka hapa uende mahali pengine, kwa maana Herode anataka kukuua.”

32. Yesu akawajibu, “Nendeni mkamwambie huyo mbweha hivi: ‘Leo na kesho ninafukuza pepo na kuponya wagonjwa, na siku ya tatu nitakamilisha kazi yangu.’

33. Hata hivyo, kwa leo, kesho na kesho kutwa, ni lazima niendelee na safari yangu, kwa sababu si sawa nabii auawe nje ya Yerusalemu.

34. “Yerusalemu! Ee Yerusalemu! Unawaua manabii na kuwapiga mawe wale waliotumwa kwako. Mara ngapi nimetaka kuwakusanya watoto wako pamoja kama kuku anavyokusanya vifaranga vyake chini ya mabawa yake, lakini hukutaka.

35. Haya! Utaachiwa mwenyewe nyumba yako. Basi, nawaambieni, hamtaniona mpaka wakati utakapofika mseme: ‘Abarikiwe huyo ajaye kwa jina la Bwana.’”

Kusoma sura kamili Luka 13