Agano la Kale

Agano Jipya

1 Wakorintho 16:11-24 Biblia Habari Njema (BHN)

11. Kwa hiyo mtu yeyote asimdharau, ila msaidieni aendelee na safari yake kwa amani ili aweze kurudi kwangu, maana mimi namngojea pamoja na ndugu zetu.

12. Kuhusu ndugu Apolo, nimemsihi sana aje kwenu pamoja na ndugu wengine, lakini hapendelei kabisa kuja sasa ila atakuja mara itakapowezekana.

13. Kesheni, simameni imara katika imani, muwe hodari na wenye nguvu.

14. Kila mfanyacho kifanyike kwa upendo.

15. Ndugu, mnaifahamu jamaa ya Stefana; wao ni watu wa kwanza kabisa kuipokea imani ya Kikristo katika Akaya, na wamejitolea kuwatumikia watu wa Mungu. Ninawasihi nyinyi ndugu zangu,

16. muufuate uongozi wa watu kama hao, na uongozi wa kila mtu afanyaye kazi na kutumika pamoja nao.

17. Nafurahi sana kwamba Stefana, Fortunato na Akaiko wamefika; wamelijaza pengo lililokuwako kwa kutokuwako kwenu.

18. Wameiburudisha roho yangu na yenu pia. Kwa hiyo inafaa kuwakumbuka watu wa namna hii.

19. Makanisa yote ya Asia yanawasalimuni. Akula na Priska pamoja na watu wote wa Mungu walio nyumbani mwao wanawasalimuni sana katika kuungana na Bwana.

20. Ndugu wote wanawasalimuni. Nanyi salimianeni kwa ishara ya mapendo ya Mungu.

21. Mimi Paulo nawasalimuni, nikiandika kwa mkono wangu mwenyewe.

22. Yeyote asiyempenda Bwana, na alaaniwe. MARANATHA – BWANA, NJOO!

23. Neema ya Bwana Yesu iwe nanyi.

24. Upendo wangu uwe kwenu katika kuungana na Kristo Yesu.

Kusoma sura kamili 1 Wakorintho 16