Agano la Kale

Agano Jipya

1 Wakorintho 14:8-23 Biblia Habari Njema (BHN)

8. La mgambo likilia bila kufuata taratibu zake, nani atajiweka tayari kwa vita?

9. Hali kadhalika na nyinyi, kama ulimi wenu hausemi kitu chenye kueleweka, nani ataweza kufahamu mnayosema? Maneno yenu yatapotea hewani.

10. Zipo lugha mbalimbali ulimwenguni, na hakuna hata mojawapo isiyo na maana.

11. Lakini ikiwa mimi sifahamu maana ya lugha asemayo mtu fulani, mimi ni mgeni kwake mtu huyo naye pia ni mgeni kwangu.

12. Hali kadhalika na nyinyi, maadamu mna hamu ya kupata vipaji vya Roho, jitahidini hasa kujipatia vile vinavyosaidia kulijenga kanisa.

13. Kwa hiyo, mwenye kunena lugha ngeni na aombe apate uwezo wa kuzifafanua.

14. Maana, nikisali kwa lugha ngeni roho yangu ndiyo inayosali, lakini akili yangu hubaki bure.

15. Nifanye nini, basi? Nitasali kwa roho yangu, nitasali pia kwa akili yangu; nitaimba kwa roho yangu, nitaimba pia kwa akili yangu.

16. Ukimsifu Mungu kwa roho yako tu, atawezaje mtu wa kawaida aliye katika mkutano kuitikia sala yako ya shukrani kwa kusema: “Amina”, kama haelewi unachosema?

17. Sala yako ya shukrani yaweza kweli kuwa bora, lakini huyo mwingine haitamfaidia.

18. Namshukuru Mungu kwamba mimi nasema kwa lugha ngeni kuliko nyinyi nyote.

19. Lakini katika mikutano ya waumini napendelea zaidi kusema maneno matano yenye kueleweka ili niwafundishe wengine, kuliko kusema maneno elfu ya lugha ngeni.

20. Ndugu, msiwe kama watoto katika fikira zenu. Kuhusu uovu, muwe kama watoto wachanga, lakini katika kufikiri ni lazima muwe kama watu waliokomaa.

21. Imeandikwa katika sheria:“Bwana asema hivi:‘Kwa njia ya wenye kunena lugha ngeni,na kwa midomo ya wageni,nitasema na watu hawa,hata hivyo, hawatanisikiliza.’”

22. Hivyo basi, kipaji cha kusema lugha ngeni ni ishara, si kwa ajili ya watu wenye imani, bali kwa ajili ya wale wasioamini; lakini kipaji cha kutangaza ujumbe wa Mungu ni kwa ajili ya wale wanaoamini na si kwa ajili ya wasioamini.

23. Basi, kanisa lote linapokutana pamoja, na wote wakaanza kusema kwa lugha ngeni, kama wakija watu wa kawaida au wasioamini, je, hawatasema kwamba nyinyi mna wazimu?

Kusoma sura kamili 1 Wakorintho 14