Agano la Kale

Agano Jipya

Yn. 4:20-39 Swahili Union Version (SUV)

20. Baba zetu waliabudu katika mlima huu, nanyi husema ya kwamba huko Yerusalemu ni mahali patupasapo kuabudia.

21. Yesu akamwambia, Mama, unisadiki, saa inakuja ambayo hamtamwabudu Baba katika mlima huu, wala kule Yerusalemu.

22. Ninyi mnaabudu msichokijua; sisi tunaabudu tukijuacho; kwa kuwa wokovu watoka kwa Wayahudi.

23. Lakini saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu.

24. Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.

25. Yule mwanamke akamwambia, Najua ya kuwa yuaja Masihi, (aitwaye Kristo); naye atakapokuja, yeye atatufunulia mambo yote.

26. Yesu akamwambia, Mimi ninayesema nawe, ndiye.

27. Mara hiyo wakaja wanafunzi wake, wakastaajabu kwa sababu alikuwa akisema na mwanamke; lakini hakuna aliyesema, Unatafuta nini? Au, Mbona unasema naye?

28. Basi yule mwanamke akauacha mtungi wake, akaenda zake mjini, akawaambia watu,

29. Njoni, mtazame mtu aliyeniambia mambo yote niliyoyatenda. Je! Haimkini huyu kuwa ndiye Kristo?

30. Basi wakatoka mjini, wakamwendea.

31. Huko nyuma wanafunzi wakamsihi wakisema, Rabi, ule.

32. Akawaambia, Mimi ninacho chakula msichokijua ninyi.

33. Basi wanafunzi wake wakasemezana, Je! Mtu amemletea chakula?

34. Yesu akawaambia, Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake.

35. Hamsemi ninyi, Bado miezi minne, ndipo yaja mavuno? Tazama, mimi nawaambieni, Inueni macho yenu myatazame mashamba, ya kuwa yamekwisha kuwa meupe, tayari kwa mavuno.

36. Naye avunaye hupokea mshahara, na kukusanya matunda kwa uzima wa milele, ili yeye apandaye na yeye avunaye wapate kufurahi pamoja.

37. Kwa maana hapo neno hilo huwa kweli, Mmoja hupanda akavuna mwingine.

38. Mimi naliwatuma myavune yale msiyoyataabikia; wengine walitaabika, nanyi mmeingia katika taabu yao.

39. Na katika mji ule Wasamaria wengi walimwamini kwa sababu ya neno la yule mwanamke, aliyeshuhudia kwamba, Aliniambia mambo yote niliyoyatenda.

Kusoma sura kamili Yn. 4