Agano la Kale

Agano Jipya

Yn. 16:1-17 Swahili Union Version (SUV)

1. Maneno hayo nimewaambia, msije mkachukizwa.

2. Watawatenga na masinagogi; naam, saa yaja atakapodhania kila mtu awauaye ya kuwa anamtolea Mungu ibada.

3. Na hayo watawatenda kwa sababu hawakumjua Baba wala mimi.

4. Lakini nimewaambia hayo, ili makusudi saa ile itakapokuja myakumbuke ya kuwa mimi naliwaambia.Sikuwaambia hayo tangu mwanzo, kwa sababu nalikuwapo pamoja nanyi.

5. Lakini sasa mimi naenda zangu kwake yeye aliyenipeleka, wala hakuna mmoja wenu aniulizaye, Unakwendapi?

6. Ila kwa sababu nimewaambia hayo huzuni imejaa mioyoni mwenu.

7. Lakini mimi nawaambia iliyo kweli; yawafaa ninyi mimi niondoke, kwa maana mimi nisipoondoka, huyo Msaidizi hatakuja kwenu; bali mimi nikienda zangu, nitampeleka kwenu.

8. Naye akiisha kuja, huyo atauhakikisha ulimwengu kwa habari ya dhambi, na haki, na hukumu.

9. Kwa habari ya dhambi, kwa sababu hawaniamini mimi;

10. kwa habari ya haki, kwa sababu mimi naenda zangu kwa Baba, wala hamnioni tena;

11. kwa habari ya hukumu, kwa sababu yule mkuu wa ulimwengu huu amekwisha kuhukumiwa.

12. Hata bado nikali ninayo mengi ya kuwaambia, lakini hamwezi kuyastahimili hivi sasa.

13. Lakini yeye atakapokuja, huyo Roho wa kweli, atawaongoza awatie kwenye kweli yote; kwa maana hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini yote atakayoyasikia atayanena, na mambo yajayo atawapasha habari yake.

14. Yeye atanitukuza mimi, kwa kuwa atatwaa katika yaliyo yangu na kuwapasha habari.

15. Na yote aliyo nayo Baba ni yangu; kwa hiyo nalisema ya kwamba atatwaa katika yaliyo yangu, na kuwapasheni habari.

16. Bado kitambo kidogo nanyi hamnioni; na tena bado kitambo kidogo nanyi mtaniona.

17. Basi baadhi ya wanafunzi wake wakasemezana, Neno gani hilo asemalo, Bado kitambo kidogo nanyi hamnioni, na tena bado kitambo kidogo nanyi mtaniona? Na hilo, Kwa sababu naenda zangu kwa Baba?

Kusoma sura kamili Yn. 16