Agano la Kale

Agano Jipya

Yn. 10:16-33 Swahili Union Version (SUV)

16. Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja.

17. Ndiposa Baba anipenda, kwa sababu nautoa uhai wangu ili niutwae tena.

18. Hakuna mtu aniondoleaye, bali mimi nautoa mwenyewe. Nami ninao uweza wa kuutoa, ninao na uweza wa kuutwaa tena. Agizo hilo nalilipokea kwa Baba yangu.

19. Kukaingia tena matengano kati ya Wayahudi, kwa ajili ya maneno hayo.

20. Wengi wao wakasema, Ana pepo huyu, tena ana wazimu; mbona mnamsikiliza?

21. Wengine wakasema, Maneno hayo siyo ya mtu mwenye pepo. Je! Pepo aweza kuwafumbua macho vipofu?

22. Basi huko Yerusalemu ilikuwa Sikukuu ya Kutabaruku; ni wakati wa baridi.

23. Naye Yesu alikuwa akitembea hekaluni, katika ukumbi wa Sulemani.

24. Basi Wayahudi walimzunguka, wakamwambia, Hata lini utatuhangaisha nafsi zetu? Kama wewe ndiwe Kristo, utuambie waziwazi.

25. Yesu akawajibu, Naliwaambia, lakini ninyi hamsadiki. Kazi hizi ninazozifanya kwa jina la Baba yangu ndizo zinazonishuhudia.

26. Lakini ninyi hamsadiki, kwa sababu hammo miongoni mwa kondoo wangu.

27. Kondoo wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua, nao wanifuata.

28. Nami nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya katika mkono wangu.

29. Baba yangu aliyenipa hao ni mkuu kuliko wote; wala hakuna mtu awezaye kuwapokonya katika mkono wa Baba yangu.

30. Mimi na Baba tu umoja.

31. Basi Wayahudi wakaokota mawe tena ili wampige.

32. Yesu akawajibu, Kazi njema nyingi nimewaonyesha, zitokazo kwa Baba; kwa ajili ya kazi ipi katika hizo mnanipiga kwa mawe?

33. Wayahudi wakamjibu, Kwa ajili ya kazi njema hatukupigi kwa mawe; bali kwa kukufuru, na kwa sababu wewe uliye mwanadamu wajifanya mwenyewe u Mungu.

Kusoma sura kamili Yn. 10