Agano la Kale

Agano Jipya

Mdo 2:22-40 Swahili Union Version (SUV)

22. Enyi waume wa Israeli, sikilizeni maneno haya: Yesu wa Nazareti, mtu aliyedhihirishwa kwenu na Mungu kwa miujiza na ajabu na ishara, ambazo Mungu alizifanya kwa mkono wake kati yenu, kama ninyi wenyewe mnavyojua;

23. mtu huyu alipotolewa kwa shauri la Mungu lililokusudiwa, na kwa kujua kwake tangu zamani, ninyi mkamsulibisha kwa mikono ya watu wabaya, mkamwua;

24. ambaye Mungu alimfufua, akiufungua uchungu wa mauti, kwa sababu haikuwezekana ashikwe nao.

25. Maana Daudi ataja habari zake,Nalimwona Bwana mbele yangu siku zote,Kwa kuwa yuko upande wa mkono wangu wa kuume, nisitikisike.

26. Kwa hiyo moyo wangu ukapendezewa,ulimi wangu ukafurahi;Tena mwili wangu nao utakaa katika matumaini.

27. Kwa maana hutaiacha roho yangu katika kuzimu;Wala hutamtoa Mtakatifu wako aone uharibifu.

28. Umenijuvisha njia za uzima;Utanijaza furaha kwa uso wako.

29. Waume, ndugu zangu, mniwie radhi, niseme kwa ujasiri mbele yenu habari za baba yetu mkuu, Daudi, ya kuwa alifariki akazikwa, na kaburi lake liko kwetu hata leo.

30. Basi kwa kuwa ni nabii, akijua ya kuwa Mungu amemwapia kwa kiapo, ya kwamba katika uzao wa viuno vyake atamketisha mmoja katika kiti chake cha enzi;

31. yeye mwenyewe akitangulia kuyaona haya, alitaja habari za kufufuka kwake Kristo, ya kwamba roho yake haikuachwa kuzimu, wala mwili wake haukuona uharibifu.

32. Yesu huyo Mungu alimfufua, na sisi sote tu mashahidi wake.

33. Basi yeye, akiisha kupandishwa hata mkono wa kuume wa Mungu, na kupokea kwa Baba ile ahadi ya Roho Mtakatifu, amekimwaga kitu hiki mnachokiona sasa na kukisikia.

34. Maana Daudi hakupanda mbinguni; bali yeye mwenyewe anasema,Bwana alimwambia Bwana wangu,Keti upande wa mkono wangu wa kuume.

35. Hata nitakapowaweka adui zako chini ya miguu yako.

36. Basi nyumba yote ya Israeli na wajue yakini ya kwamba Mungu amemfanya Yesu huyo mliyemsulibisha kuwa Bwana na Kristo.

37. Walipoyasikia haya wakachomwa mioyo yao, wakamwambia Petro na mitume wengine, Tutendeje, ndugu zetu?

38. Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu.

39. Kwa kuwa ahadi hii ni kwa ajili yenu, na kwa watoto wenu, na kwa watu wote walio mbali, na kwa wote watakaoitwa na Bwana Mungu wetu wamjie.

40. Akawashuhudia kwa maneno mengine mengi sana na kuwaonya, akisema, Jiokoeni na kizazi hiki chenye ukaidi.

Kusoma sura kamili Mdo 2