Agano la Kale

Agano Jipya

Mdo 2:18-29 Swahili Union Version (SUV)

18. Naam, na siku zile nitawamwagia watumishi wangu wanaume na wanawake Roho yangu, nao watatabiri.

19. Nami nitatoa ajabu katika mbingu juu, na ishara katika nchi chini, damu na moto, na mvuke wa moshi.

20. Jua litageuka kuwa giza, na mwezi kuwa damu, kabla ya kuja ile siku ya Bwana iliyo kuu na iliyo dhahiri.

21. Na itakuwa kila atakayeliitia jina la Bwana ataokolewa.

22. Enyi waume wa Israeli, sikilizeni maneno haya: Yesu wa Nazareti, mtu aliyedhihirishwa kwenu na Mungu kwa miujiza na ajabu na ishara, ambazo Mungu alizifanya kwa mkono wake kati yenu, kama ninyi wenyewe mnavyojua;

23. mtu huyu alipotolewa kwa shauri la Mungu lililokusudiwa, na kwa kujua kwake tangu zamani, ninyi mkamsulibisha kwa mikono ya watu wabaya, mkamwua;

24. ambaye Mungu alimfufua, akiufungua uchungu wa mauti, kwa sababu haikuwezekana ashikwe nao.

25. Maana Daudi ataja habari zake,Nalimwona Bwana mbele yangu siku zote,Kwa kuwa yuko upande wa mkono wangu wa kuume, nisitikisike.

26. Kwa hiyo moyo wangu ukapendezewa,ulimi wangu ukafurahi;Tena mwili wangu nao utakaa katika matumaini.

27. Kwa maana hutaiacha roho yangu katika kuzimu;Wala hutamtoa Mtakatifu wako aone uharibifu.

28. Umenijuvisha njia za uzima;Utanijaza furaha kwa uso wako.

29. Waume, ndugu zangu, mniwie radhi, niseme kwa ujasiri mbele yenu habari za baba yetu mkuu, Daudi, ya kuwa alifariki akazikwa, na kaburi lake liko kwetu hata leo.

Kusoma sura kamili Mdo 2