Agano la Kale

Agano Jipya

Ebr. 2:1-13 Swahili Union Version (SUV)

1. Kwa hiyo imetupasa kuyaangalia zaidi hayo yaliyosikiwa tusije tukayakosa.

2. Kwa maana, ikiwa lile neno lililonenwa na malaika lilikuwa imara, na kila kosa na uasi ulipata ujira wa haki,

3. sisi je! Tutapataje kupona, tusipojali wokovu mkuu namna hii? Ambao kwanza ulinenwa na Bwana, kisha ukathibitika kwetu na wale waliosikia;

4. Mungu naye akishuhudu pamoja nao kwa ishara na ajabu na nguvu za namna nyingi, na kwa magawanyo ya Roho Mtakatifu, kama alivyopenda mwenyewe.

5. Maana hakuuweka chini ya malaika ulimwengu ule ujao tunaounena, ila mtu mmoja ameshuhudia hivi mahali fulani, akisema,

6. Mwanadamu ni nini hata umkumbuke,Ama mwana wa binadamu, hata umwangalie?

7. Umemfanya mdogo punde kuliko malaika,Umemvika taji ya utukufu na heshima,Umemtawaza juu ya kazi za mikono yako;

8. Umeweka vitu vyote chini ya nyayo zake.Kwa maana katika kuweka vitu vyote chini yake hakusaza kitu kisichowekwa chini yake. Lakini sasa bado hamjaona vitu vyote kutiwa chini yake,

9. ila twamwona yeye aliyefanywa mdogo punde kuliko malaika, yaani, Yesu, kwa sababu ya maumivu ya mauti, amevikwa taji ya utukufu na heshima, ili kwa neema ya Mungu aionje mauti kwa ajili ya kila mtu.

10. Kwa kuwa ilimpasa yeye, ambaye kwa ajili yake na kwa njia yake vitu vyote vimekuwapo, akileta wana wengi waufikilie utukufu, kumkamilisha kiongozi mkuu wa wokovu wao kwa njia ya mateso.

11. Maana yeye atakasaye na hao wanaotakaswa wote pia watoka kwa mmoja. Kwa ajili hii haoni haya kuwaita ndugu zake;

12. akisema,Nitalihubiri jina lako kwa ndugu zangu;Katikati ya kanisa nitakuimbia sifa.

13. Na tena,Nitakuwa nimemtumaini yeye.Na tena,Tazama, mimi nipo hapa na watoto niliopewa na Mungu.

Kusoma sura kamili Ebr. 2