Agano la Kale

Agano Jipya

Zaburi 18:2-22 Biblia Habari Njema (BHN)

2. Mwenyezi-Mungu ni mwamba wangu,ngome yangu na mkombozi wangu;Mungu wangu, mwamba wangu ninayemkimbilia usalama;ngao yangu, nguvu za wokovu wangu na ngome yangu.

3. Namwita Mwenyezi-Mungu astahiliye sifa anisaidie,nami naokolewa kutoka kwa maadui zangu.

4. Kamba za kifo zilinizingira,mawimbi ya maangamizi yalinivamia;

5. kamba za kuzimu zilinizinga,mitego ya kifo ilinikabili.

6. Katika taabu yangu nilimwita Mwenyezi-Mungu,nilimlilia Mungu wangu anisaidie.Aliisikia sauti yangu hekaluni mwake;kilio changu kilimfikia masikioni mwake.

7. Hapo dunia ikatetemeka na kutikisika;misingi ya milima ikayumbayumba,kwani Mungu alikuwa amekasirika.

8. Moshi ulifuka kutoka puani mwake,moto uunguzao ukatoka kinywani mwake;makaa ya moto yalilipuka kutoka kwake.

9. Aliinamisha anga, akashuka chini;na wingu jeusi chini ya miguu yake.

10. Alipanda kiumbe chenye mabawa akaruka;akapaa kasi juu ya mabawa ya upepo.

11. Alijifunika giza pande zote,mawingu mazito yaliyojaa maji yalimzunguka.

12. Umeme ulimulika mbele yake;kukatokea mawinguni mvua ya mawe na makaa ya moto.

13. Mwenyezi-Mungu alinguruma kutoka mbinguni;Mungu Mkuu akatoa sauti yake,kukatokea mvua ya mawe na makaa ya moto.

14. Aliwapiga maadui mishale yake, akawatawanya,alirusha umeme, akawatimua.

15. Ulipowakemea maadui zako ee Mwenyezi-Mungu,ulipowatisha kwa ghadhabu yako,vilindi vya bahari vilifunuliwa,misingi ya dunia ikaonekana.

16. Mungu alinyosha mkono kutoka juu akanichukua,kutoka katika maji mengi alininyanyua.

17. Aliniokoa kutoka kwa maadui zangu wenye nguvu nyingi,aliniokoa kutoka kwa hao walionichukia,maana walikuwa na nguvu kunishinda.

18. Walinivamia nilipokuwa taabuni,lakini Mwenyezi-Mungu alikuwa kinga yangu.

19. Alinileta, akaniweka mahali pa usalama;alinisalimisha, kwani alipendezwa nami.

20. Mwenyezi-Mungu alinipa tuzo kadiri ya uadilifu wangu;alinituza kwa vile mikono yangu haina hatia.

21. Maana nimefuata njia za Mwenyezi-Mungu,wala sikujitenga na Mungu wangu kwa uovu.

22. Nimeshika maagizo yake yote,sikuacha kufuata masharti yake.

Kusoma sura kamili Zaburi 18