Agano la Kale

Agano Jipya

Yeremia 35:1-13 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Neno la Mwenyezi-Mungu lililomjia Yeremia wakati wa utawala wa Yehoyakimu mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda:

2. “Nenda nyumbani kwa Warekabu, ukaongee nao. Kisha, walete katika chumba kimojawapo cha nyumba yangu mimi Mwenyezi-Mungu, uwape divai wanywe.”

3. Basi, nikamchukua Yaazania mwana wa Yeremia, mwana wa Habazinia, na ndugu zake pamoja na wanawe wote na ukoo wote wa Warekabu,

4. nikawaleta kwenye nyumba ya Mwenyezi-Mungu, katika chumba cha wana wa Hanani mwana wa Igdalia, mtu wa Mungu. Chumba hicho kilikuwa karibu na ukumbi wa wakuu, juu ya ukumbi wa Maaseya mwana wa Shalumu, mlinzi wa ukumbi.

5. Kisha nikaleta vikombe na mabakuli yaliyojaa divai mbele ya hao Warekabu, nikawaambia, “Kunyweni divai.”

6. Lakini wao wakajibu, “Sisi hatunywi divai, maana Yonadabu mwana wa Rekabu, mzee wetu, alituamuru hivi: ‘Msinywe divai; msinywe nyinyi wenyewe binafsi wala wana wenu milele.

7. Msijenge nyumba, msilime mashamba, wala msiwe na shamba la mizabibu. Lakini mtaishi katika mahema siku zote za maisha yenu, ili mpate kuishi siku nyingi katika nchi mnamoishi kama wageni.’

8. Sisi tumeitii daima amri hiyo ya mzee wetu Yonadabu mwana wa Rekabu, kuhusu jambo alilotuamuru. Sisi hatunywi kamwe divai; sisi wenyewe hatunywi, wala wake zetu, wala watoto wetu wa kiume au wa kike.

9. Sisi hatujijengei nyumba za kuishi. Hatuna mashamba ya mizabibu wala mashamba ya kulima na kupanda mbegu.

10. Sisi tumeishi katika mahema na kutii mambo yote ambayo Yonadabu, mzee wetu, alituamuru.

11. Lakini Nebukadneza, mfalme wa Babuloni alipofika, kuishambulia nchi hii, tuliamua kuja Yerusalemu ili tuliepe jeshi la Wakaldayo na la Waashuru. Kwa hiyo sasa tunaishi mjini Yerusalemu.”

12. Kisha neno la Mwenyezi-Mungu likamjia Yeremia:

13. “Mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, nasema hivi: Nenda ukawaambie watu wa Yuda na wakazi wa Yerusalemu hivi: Je, nyinyi hamwezi kupokea mafundisho na kusikia maneno yangu?

Kusoma sura kamili Yeremia 35