Agano la Kale

Agano Jipya

Yeremia 18:1-10 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Neno la Mwenyezi-Mungu lilinijia:

2. “Yeremia, inuka uende nyumbani kwa mfinyanzi, na huko nitakupa maneno yangu.”

3. Basi, nikateremka mpaka nyumbani kwa mfinyanzi, nikamkuta mfinyanzi akifanya kazi yake penye gurudumu la kufinyangia.

4. Na ikawa kwamba chombo alichokifinyanga kilipoharibika mikononi mwake, yeye alifinyanga upya chombo kingine kadiri ilivyompendeza.

5. Kisha, neno la Mwenyezi-Mungu likanijia:

6. “Enyi Waisraeli! Je, mimi Mwenyezi-Mungu siwezi kuwafanya nyinyi kama alivyofanya mfinyanzi huyu? Jueni kuwa kama ulivyo udongo mikononi mwa mfinyanzi, ndivyo nyinyi mlivyo mikononi mwangu.

7. Wakati wowote nitakapotoa tamko kuhusu taifa au ufalme kwamba nitalingoa na kulivunja na kuliangamiza,

8. halafu taifa hilo likageuka na kuacha uovu wake, basi, mimi nitaacha kulitendea yale mambo niliyokusudia kulitendea.

9. Hali kadhalika, wakati wowote nikitoa tamko kuhusu taifa au ufalme kwamba nitalijenga na kulistawisha,

10. kisha taifa hilo likafanya uovu mbele yangu na kukataa kunitii, basi, mimi nitaacha kulitendea mema hayo niliyokusudia kulitendea.

Kusoma sura kamili Yeremia 18