Agano la Kale

Agano Jipya

Walawi 3:7-17 Biblia Habari Njema (BHN)

7. Kama mtu atatoa mwanakondoo kuwa sadaka yake, basi, atamtolea mbele ya Mwenyezi-Mungu,

8. akiweka mkono wake juu ya kichwa cha mnyama huyo na kumchinja mbele ya hema la mkutano. Makuhani wazawa wa Aroni watainyunyizia madhabahu damu yake pande zake zote.

9. Kisha, kutoka katika sadaka hiyo ya amani anayotolewa Mwenyezi-Mungu kwa moto, atamtolea sehemu zifuatazo: Mafuta yake, mkia wenye mafuta mzima uliokatwa karibu kabisa na uti wa mgongo pamoja na mafuta yote yanayofunika matumbo na mafuta yote yaliyo kwenye matumbo,

10. zile figo mbili na mafuta yake pamoja na sehemu bora ya ini.

11. Kuhani ataviteketeza hivyo vyote juu ya madhabahu kama chakula anachotolewa Mwenyezi-Mungu kwa moto.

12. “Kama sadaka yake ni mbuzi, basi, atamtolea mbele ya Mwenyezi-Mungu

13. akiweka mkono wake juu ya kichwa cha mnyama huyo na kumchinja mbele ya hema la mkutano. Wazawa wa Aroni watainyunyizia madhabahu damu yake pande zake zote.

14. Kisha, mafuta yote yanayofunika matumbo

15. na zile figo mbili na mafuta yake pamoja na sehemu bora ya ini, atamtolea Mwenyezi-Mungu sadaka ya kuteketezwa kwa moto.

16. Kuhani ataviteketeza juu ya madhabahu kama chakula kinachotolewa kwa Mwenyezi-Mungu kwa moto kutoa harufu ya kumpendeza Mungu. Mafuta yote ni ya Mwenyezi-Mungu.

17. Ndiyo maana siku zote na mahali popote mtakapokaa ni lazima kushika kanuni hii. Kamwe msile mafuta wala damu.”

Kusoma sura kamili Walawi 3