Agano la Kale

Agano Jipya

Walawi 21:1-12 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose, “Waambie makuhani, wana wa Aroni, kwamba pasiwe na mtu yeyote miongoni mwao atakayejitia najisi kwa kugusa maiti ya watu wa jamaa yake,

2. isipokuwa kama ni maiti ya ndugu yake wa karibu, yaani mama yake, baba yake, mwanawe, binti yake, ndugu yake

3. au dada yake ambaye (aliye wa jamaa yake ya karibu), naye hajaolewa bado.

4. Yeye, akiwa mwenye madaraka katika jamaa yake, asijitie unajisi.

5. Wazawa wa Aroni kamwe wasijinyoe upara kuomboleza wala wasikate pembe za ndevu zao wala kujichanja chale mwilini.

6. Watakuwa watakatifu kwa Mungu wao wala wasilikufuru jina la Mungu wao. Maana wao ndio wanaotolea zile sadaka anazopewa Mwenyezi-Mungu kwa moto yaani chakula cha Mungu. Basi, ni lazima wawe watakatifu.

7. Kwa kuwa kuhani amewekwa wakfu kwa Mungu wake, kamwe asioe kahaba, wala mwanamke asiye bikira wala aliyepewa talaka.

8. Utamtambua kuhani kuwa aliyewekwa wakfu, maana yeye ndiye anayetoa sadaka ya mkate wa Mungu wako; utamtambua kuwa mtakatifu, maana mimi Mwenyezi-Mungu ninayekuweka wewe wakfu, ni mtakatifu.

9. Binti wa kuhani yeyote akijitia unajisi kwa kufanya ukahaba, atateketezwa kwa moto kwani anamtia baba yake unajisi.

10. “Kuhani mkuu yeyote, kwa kuwa yeye ni mkuu kati ya ndugu zake, naye amemiminiwa mafuta ya kupaka kichwani pake, na kuwekwa wakfu ili ayavae mavazi matakatifu, asiache nywele zake kuwa ovyo wala asirarue mavazi yake kuomboleza.

11. Asikaribie maiti wala kujitia unajisi kwa maiti hata kama ni ya baba yake au ya mama yake.

12. Kwa kuwa amewekwa wakfu kwa kupakwa mafuta ya Mungu wake kichwani, basi asiondoke mahali patakatifu wala asipatie unajisi. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

Kusoma sura kamili Walawi 21