Agano la Kale

Agano Jipya

Ruthu 4:11-22 Biblia Habari Njema (BHN)

11. Basi wazee waliokuwa langoni na watu wote waliokuwapo walijibu, “Ndiyo, sisi ni mashahidi. Mwenyezi-Mungu amfanye mke wako awe kama Raheli na Lea, ambao wote wawili waliijenga nyumba ya Israeli. Nawe upate kustawi katika jamaa ya Efratha, uwe na sifa katika Bethlehemu.

12. Kwa sababu ya watoto Mwenyezi-Mungu atakaokupatia ambao mwanamke huyu atakuzalia, nayo nyumba yako iwe kama nyumba ya Peresi ambaye Tamari alimzalia Yuda.”

13. Kwa hiyo, Boazi akamchukua Ruthu akawa mke wake. Mwenyezi-Mungu alimjalia Ruthu naye akachukua mimba, akajifungua mtoto wa kiume.

14. Ndipo wanawake wa mji huo wakamwambia Naomi, “Atukuzwe Mwenyezi-Mungu ambaye hakukuacha leo bila kuwa na jamaa aliye karibu wa kukutunza; naye awe mwenye sifa kubwa katika Israeli.

15. Yeye atakurudishia uhai wako na atakutunza katika uzee wako; maana mkwe wako anayekupenda ambaye ana thamani kubwa zaidi kwako kuliko watoto wa kiume saba, ndiye amemzaa.”

16. Basi Naomi alimchukua mtoto huyo akamweka kifuani mwake na kumlea.

17. Wanawake majirani walimwita mtoto huyo Obedi wakisema, “Mtoto amezaliwa kwa Naomi.” Hatimaye Obedi akamzaa Yese aliyemzaa Daudi.

18. Na hivi ndivyo vizazi vya Peresi: Peresi alimzaa Hesroni,

19. Hesroni akamzaa Rami, Rami akamzaa Aminadabu,

20. Aminadabu akamzaa Nahshoni, Nahshoni akamzaa Salmoni,

21. Salmoni akamzaa Boazi, Boazi akamzaa Obedi,

22. Obedi akamzaa Yese na Yese akamzaa Daudi.

Kusoma sura kamili Ruthu 4