Agano la Kale

Agano Jipya

Mwanzo 4:15-26 Biblia Habari Njema (BHN)

15. Lakini Mwenyezi-Mungu akamjibu, “Sivyo! Atakayekuua wewe Kaini atalipizwa mara saba.” Basi, Mwenyezi-Mungu akamtia Kaini alama ya tahadhari, ili yeyote atakayemwona asimuue.

16. Kisha Kaini akaondoka mbele ya Mwenyezi-Mungu, akawa anaishi katika nchi ya Nodi, upande wa mashariki wa Edeni.

17. Kaini akalala na mkewe, naye akapata mimba, akamzaa Henoki. Kaini akajenga mji akauita kwa jina la Henoki mwanawe.

18. Henoki akamzaa Iradi, naye Iradi akamzaa Mehuyaeli; Mehuyaeli akamzaa Methushaeli, naye Methushaeli akamzaa Lameki.

19. Lameki alioa wanawake wawili, mmoja aliitwa Ada na mwingine Sila.

20. Ada alimzaa Yabali ambaye alikuwa baba yao wafugaji waishio mahemani.

21. Ndugu yake alikuwa Yubali; huyo alikuwa baba yao wanamuziki wote wapigao zeze na filimbi.

22. Sila naye alimzaa Tubal-kaini, ambaye alikuwa mhunzi wa vyombo vyote vya shaba na chuma. Dada yake Tubal-kaini alikuwa Naama.

23. Lameki akawaambia wake zake,“Ada na Sila sikieni sauti yangu!Sikilizeni nisemayo enyi wake za Lameki.Mimi niliua mtu kwa kunijeruhi,naam, nilimuua kijana kwa kuniumiza.

24. Ikiwa Kaini atalipizwa mara saba,kweli Lameki atalipizwa mara sabini na saba.”

25. Adamu akalala tena na Hawa mkewe, naye akazaa mtoto wa kiume, akamwita Sethi akisema, “Mungu amenijalia mtoto mahali pa Abeli aliyeuawa na Kaini.”

26. Sethi naye alipata mtoto wa kiume, akamwita Enoshi. Hapo ndipo watu walipoanza kumwomba Mwenyezi-Mungu kwa jina lake.

Kusoma sura kamili Mwanzo 4