Agano la Kale

Agano Jipya

Mwanzo 39:13-23 Biblia Habari Njema (BHN)

13. Hapo, yule mwanamke alipoona kwamba Yosefu ameliacha vazi lake mikononi mwake na kukimbilia nje,

14. akawaita watumishi wa nyumbani mwake na kuwaambia, “Tazameni! Huyu Mwebrania tuliyeletewa anatuaibisha. Alikuja kwangu akitaka kunishika kwa nguvu, lakini nikapiga kelele.

15. Aliposikia napiga kelele, aliliacha vazi lake, akakimbilia nje!”

16. Basi, yule mwanamke akaliweka vazi hilo mpaka mumewe aliporudi nyumbani.

17. Akamsimulia kisa kile akisema, “Huyu mtumishi Mwebrania uliyemleta kwetu alinijia ili kuniaibisha.

18. Lakini mara tu nilipopiga kelele, aliliacha vazi lake na kukimbilia nje.”

19. Basi, bwana wake Yosefu alipoyasikia maneno ya mkewe, kwamba ndivyo mtumishi wake alivyomtendea, akawaka hasira,

20. akamchukua Yosefu na kumtia gerezani, mahali walipofungwa wahalifu wa mfalme.

21. Lakini hata humo gerezani Mwenyezi-Mungu alikuwa pamoja na Yosefu akimfadhili hata kumfanya apendeke mbele ya mkuu wa gereza.

22. Hivyo mkuu wa gereza alimweka Yosefu awe mkuu wa wafungwa wote humo gerezani; kila kitu kilichofanyika humo kilifanywa kwa mamlaka yake.

23. Huyo mkuu wa gereza hakujishughulisha tena na kitu chochote alichokabidhiwa Yosefu kwa maana Mwenyezi-Mungu alikuwa pamoja na Yosefu na kufanikisha kila kitu alichofanya.

Kusoma sura kamili Mwanzo 39