Agano la Kale

Agano Jipya

Mwanzo 35:9-19 Biblia Habari Njema (BHN)

9. Baada ya Yakobo kurudi kutoka Padan-aramu, Mungu alimtokea tena na kumbariki.

10. Mungu alimwambia, “Jina lako ni Yakobo, lakini hutaitwa hivyo tena, bali sasa jina lako litakuwa Israeli.” Kwa hiyo Yakobo akaitwa Israeli.

11. Tena Mungu akamwambia, “Mimi ndimi Mungu mwenye nguvu. Ujaliwe wazawa wengi; kwako wewe kutatokea taifa, mataifa na wafalme.

12. Nchi niliyowapa Abrahamu na Isaka, nitakupa wewe na wazawa wako.”

13. Basi, baada ya kuongea na Yakobo, Mungu akamwacha na kupanda juu.

14. Yakobo akasimika nguzo ya jiwe la ukumbusho mahali hapo Mungu alipozungumza naye, akaiweka wakfu kwa kuimiminia tambiko ya kinywaji na mafuta.

15. Basi, Yakobo akapaita mahali hapo alipozungumza na Mungu Betheli.

16. Yakobo na jamaa yake yote waliendelea na safari yao kutoka Betheli. Walipokuwa umbali fulani kabla ya kufika Efratha, Raheli akashikwa na uchungu mkali wa kuzaa.

17. Naye alipokuwa katika uchungu huo, mkunga akamwambia, “Usiogope, umepata mtoto mwingine wa kiume.”

18. Raheli huku akikata roho, akampa huyo mtoto jina Ben-oni. Lakini baba yake akamwita mtoto huyo Benyamini.

19. Basi, Raheli akafariki na kuzikwa kando ya njia iendayo Efratha (yaani Bethlehemu).

Kusoma sura kamili Mwanzo 35