Agano la Kale

Agano Jipya

Mwanzo 35:14-29 Biblia Habari Njema (BHN)

14. Yakobo akasimika nguzo ya jiwe la ukumbusho mahali hapo Mungu alipozungumza naye, akaiweka wakfu kwa kuimiminia tambiko ya kinywaji na mafuta.

15. Basi, Yakobo akapaita mahali hapo alipozungumza na Mungu Betheli.

16. Yakobo na jamaa yake yote waliendelea na safari yao kutoka Betheli. Walipokuwa umbali fulani kabla ya kufika Efratha, Raheli akashikwa na uchungu mkali wa kuzaa.

17. Naye alipokuwa katika uchungu huo, mkunga akamwambia, “Usiogope, umepata mtoto mwingine wa kiume.”

18. Raheli huku akikata roho, akampa huyo mtoto jina Ben-oni. Lakini baba yake akamwita mtoto huyo Benyamini.

19. Basi, Raheli akafariki na kuzikwa kando ya njia iendayo Efratha (yaani Bethlehemu).

20. Yakobo akasimika nguzo ya kumbukumbu juu ya kaburi la Raheli ambayo ipo mpaka leo.

21. Israeli akaendelea na safari yake na kupiga kambi yake baada ya kuupita mnara wa Ederi.

22. Wakati Israeli alipokuwa anakaa nchini humo, mwanawe Reubeni, alilala na Bilha, suria wa baba yake; naye Israeli akasikia habari hizo.Yakobo alikuwa na watoto wa kiume kumi na wawili.

23. Wana wa Lea walikuwa Reubeni, mzaliwa wa kwanza wa Yakobo, Simeoni, Lawi, Yuda, Isakari na Zebuluni.

24. Watoto wa kiume wa Raheli walikuwa Yosefu na Benyamini.

25. Watoto wa kiume waliozaliwa na Bilha, mjakazi wa Raheli, walikuwa Dani na Naftali.

26. Na watoto wa kiume waliozaliwa na Zilpa, mjakazi wa Lea, walikuwa Gadi na Asheri. Hao ndio watoto wa kiume wa Yakobo, aliowazaa alipokuwa kule Padan-aramu.

27. Yakobo aliondoka akaenda Mamre kwa baba yake Isaka, huko Kiriath-arba, yaani Hebroni, mahali ambapo Abrahamu na Isaka walikaa kama wageni.

28. Isaka alikuwa na miaka 180

29. akafariki akiwa mzee wa miaka mingi. Watoto wake, Esau na Yakobo wakamzika.

Kusoma sura kamili Mwanzo 35