Agano la Kale

Agano Jipya

Mwanzo 30:11-22 Biblia Habari Njema (BHN)

11. Lea akasema, “Bahati njema.” Kwa hiyo akamwita mtoto huyo Gadi.

12. Zilpa, mtumishi wa Lea, alimzalia Yakobo mtoto wa pili wa kiume.

13. Lea akasema, “Bahati njema! Sasa wanawake wataniita heri.” Kwa hiyo akamwita mtoto huyo Asheri.

14. Ikawa wakati wa mavuno ya ngano, Reubeni alikwenda shambani na huko akapata tunguja, akamletea mama yake Lea. Raheli akamwambia Lea, “Tafadhali, nipe baadhi ya tunguja za mwanao.”

15. Lakini Lea akamsemea kwa ukali, “Je, unadhani ni jambo dogo kuninyanganya mume wangu, na sasa unataka kuchukua tunguja za mwanangu?” Raheli akamjibu, “Ikiwa utanipa tunguja za mwanao, Yakobo atalala kwako leo.”

16. Basi, jioni Yakobo alipokuwa anarudi toka shambani, Lea alitoka kwenda kumlaki, akamwambia, “Leo huna budi kulala nami, kwani nimekuajiri kwa tunguja za mwanangu.” Hivyo Yakobo akalala kwa Lea usiku huo.

17. Mungu akasikiliza ombi la Lea, naye akapata mimba na kumzalia Yakobo mtoto wa tano wa kiume.

18. Lea akasema, “Mungu amenipa ujira wangu kwa sababu nilimpa mume wangu mjakazi wangu.” Kwa hiyo akamwita mtoto huyo Isakari.

19. Lea akapata mimba tena na kumzalia Yakobo mtoto wa sita wa kiume.

20. Akasema, “Mungu amenipa zawadi bora. Sasa mume wangu ataniheshimu kwa maana nimemzalia watoto sita wa kiume.” Kwa hiyo akamwita mtoto huyo Zebuluni.

21. Baadaye akazaa mtoto wa kike, akamwita Dina.

22. Kisha Mungu akamkumbuka Raheli, akalikubali ombi lake na kumjalia kupata watoto.

Kusoma sura kamili Mwanzo 30