Agano la Kale

Agano Jipya

Mwanzo 27:34-45 Biblia Habari Njema (BHN)

34. Esau alipoyasikia maneno ya baba yake, akaangua kilio cha uchungu. Kisha akamwambia baba yake, “Ee baba yangu, nibariki na mimi, tafadhali!”

35. Lakini Isaka akasema, “Ndugu yako alikuja kwa hila, naye amechukua baraka yako.”

36. Esau akasema, “Ndio maana anaitwa Yakobo! Amechukua nafasi yangu mara mbili. Kwanza alichukua haki yangu ya mzaliwa wa kwanza, na sasa amechukua baraka Zangu.” Kisha akamwuliza baba yake, “Je, hukunibakizia baraka yoyote?”

37. Isaka akamjibu, “Nimekwisha mfanya Yakobo kuwa mtawala wako, na kumpa ndugu zake wote kuwa watumishi wake. Nimempatia nafaka na divai. Nikufanyie nini sasa, wewe mwanangu?”

38. Esau akamwambia baba yake, “Baba, kwani una baraka moja tu? Nibariki hata mimi, ee baba!” Hapo Esau akalia kwa sauti kubwa.

39. Ndipo Isaka, baba yake, akamwambia,“Makao yako yatakuwa mbali na ardhi yenye rutuba,na mbali na umande wa mbinguni.

40. Utaishi kwa upanga wako,na utamtumikia ndugu yako;lakini utakapoasiutaivunja kongwa yake shingoni mwako.”

41. Basi, Esau akamchukia Yakobo kwa sababu ya baraka aliyokuwa amepewa na baba yake. Esau akawaza, “Siku za matanga ya baba zitakapokwisha, ndipo nitakapomuua ndugu yangu Yakobo.”

42. Lakini Rebeka alipojua nia ya mwanawe mkubwa, akamwita mwanawe mdogo Yakobo, akamwambia, “Jihadhari, ndugu yako Esau anajifariji kwa kupanga kukuua.

43. Kwa hiyo, mwanangu, sikiliza maneno yangu. Ondoka ukimbilie kwa kaka yangu Labani kule Harani.

44. Kaa naye kwa muda, mpaka ghadhabu ya nduguyo itakapopoa.

45. Ghadhabu yake itakapopoa, naye atakapokuwa amesahau uliyomtendea, nitatuma mtu akurudishe. Kwa nini nifiwe na nyinyi wote wawili siku moja?”

Kusoma sura kamili Mwanzo 27