Agano la Kale

Agano Jipya

Mwanzo 24:22-32 Biblia Habari Njema (BHN)

22. Ngamia walipotosheka kunywa maji, yule mtu akampa huyo msichana pete ya dhahabu yenye uzito upatao gramu sita, na bangili mbili za dhahabu za gramu kumi kila moja.

23. Akamwuliza, “Niambie tafadhali: Wewe ni binti nani? Je, kuna nafasi ya kulala nyumbani kwenu?”

24. Rebeka akajibu, “Mimi ni binti Bethueli, mwana wa Milka, mkewe Nahori.

25. Kwetu kuna majani na malisho ya kutosha na mahali pa kulala wageni.”

26. Ndipo yule mtu akainamisha kichwa chake, akamwabudu Mwenyezi-Mungu

27. akisema, “Atukuzwe Mwenyezi-Mungu, Mungu wa bwana wangu Abrahamu, ambaye hajasahau fadhili zake na uaminifu wake kwa bwana wangu. Mwenyezi-Mungu ameniongoza mimi mwenyewe moja kwa moja hadi kwa jamaa ya bwana wangu!”

28. Kisha yule msichana akakimbia kwenda kuwapa habari jamaa za mama yake.

29. Rebeka alikuwa na kaka yake aitwaye Labani. Labani akatoka mbio kukutana na yule mtu kisimani.

30. Labani alikuwa ameiona ile pete na bangili mikononi mwa dada yake, na kusikia mambo Rebeka aliyoambiwa na huyo mtu. Labani alimkuta yule mtu amesimama karibu na ngamia wake kando ya kisima.

31. Labani akamwambia, “Karibu kwetu wewe uliyebarikiwa na Mwenyezi-Mungu. Mbona unasimama nje? Mimi mwenyewe nimekwisha tayarisha nyumba na mahali kwa ajili ya hawa ngamia wako!”

32. Basi, mtumishi huyo wa Abrahamu akaingia nyumbani. Labani akawafungua ngamia na kuwapatia majani ngamia wake, akampa yeye na watu wake maji ya kunawa miguu.

Kusoma sura kamili Mwanzo 24