Agano la Kale

Agano Jipya

Kutoka 9:9-18 Biblia Habari Njema (BHN)

9. Majivu hayo yatakuwa vumbi nyembamba itakayoenea juu ya nchi yote ya Misri. Yatasababisha majipu yatakayotumbuka na kuwa vidonda kwa watu na wanyama kila mahali nchini Misri.”

10. Basi, wakachukua majivu kutoka kwenye tanuri, wakamwendea Farao, naye Mose akayarusha juu hewani.

11. Watu na wanyama wakavamiwa na majipu hata wale wachawi hawakuweza kujitokeza maana wao pamoja na Wamisri wote pia walivamiwa na majipu hayo.

12. Lakini Mwenyezi-Mungu akamfanya Farao kuwa mkaidi, naye hakuwasikiliza kama vile Mwenyezi-Mungu alivyomwambia Mose.

13. Kisha, Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, “Kesho, amka alfajiri na mapema umwendee Farao, umwambie kwamba mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Waebrania, nasema hivi, ‘Waache watu wangu waondoke ili wakanitumikie.

14. Maana safari hii, wewe mwenyewe, maofisa wako na watu wako mtakumbana na mapigo yangu makali. Nawe utatambua kwamba hakuna yeyote duniani aliye kama mimi.

15. Ningalikwisha kukuangamiza tayari wewe na watu wako kwa maradhi mabaya, nanyi mngalikuwa mmekwisha angamia.

16. Lakini nimewaacheni muishi ili kudhihirisha uwezo wangu. Kwa hiyo dunia yote itatambua kuwa mimi ni nani.

17. Lakini bado unaonesha kiburi dhidi ya watu wangu, wala huwaachi waondoke.

18. Kwa hiyo kesho, wakati kama huu, nitaleta mvua kubwa ya mawe ambayo haijawahi kutokea nchini Misri, tangu mwanzo wake hadi leo.

Kusoma sura kamili Kutoka 9