Agano la Kale

Agano Jipya

Kutoka 21:5-24 Biblia Habari Njema (BHN)

5. Lakini kama mtumwa huyo akisema kwamba anampenda bwana wake, mke wake na watoto wake na hataki kuondoka na kuwa huru,

6. basi, bwana wake atamleta mbele ya Mungu. Kisha atampeleka kwenye mlango au kizingitini na kumtoboa sikio lake kwa shazia; naye atamtumikia bwana wake maisha yake yote.

7. “Mtu akimwuza binti yake kuwa mtumwa, huyo hatapata uhuru wake kama watumwa wa kiume.

8. Ikiwa huyo bwana wake alimnunua awe mmoja wa wake zake, kisha asipendezwe naye, huyo bwana atamwacha baba yake huyo mtumwa amkomboe. Huyo bwana hana haki ya kumwuza kwa watu wa mataifa mengine, kwa kuwa atakuwa amekosa uaminifu.

9. Kama ataamua kumwoza kwa mwanawe, atamtendea mtumwa huyo kama binti yake.

10. Kama huyo bwana akioa mke mwingine, lazima aendelee kumtosheleza mkewe wa kwanza kwa chakula, mavazi na haki zake za ndoa.

11. Iwapo huyo bwana hatamtimizia haki hizo tatu, basi, mke ataondoka na kuwa huru bila malipo yoyote.

12. “Ampigaye mtu na kumwua, lazima auawe.

13. Lakini kama hakuwa amemvizia, bali ni kwa ajali, basi, huyo mwuaji ataweza kukimbilia usalama mahali nitakapowachagulieni.

14. Lakini mtu akimshambulia mwenzake makusudi na kumwua kwa ujeuri, hata kama atakimbilia kwenye madhabahu, mtamtoa huko madhabahuni pangu na kumwua.

15. “Ampigaye baba yake au mama yake lazima auawe.

16. “Amtekaye mtu nyara ili kumwuza au kumfanya mtumwa wake lazima auawe.

17. “Amlaaniye baba yake au mama yake lazima auawe.

18. “Watu wawili wakigombana, kisha mmoja akampiga mwenzake jiwe au ngumi bila kumwua, lakini akamjeruhi kiasi cha kumfanya augue na kulala kitandani,

19. iwapo huyo aliyepigwa atapata nafuu na kuweza kutembea kwa kutegemea fimbo, huyo aliyemjeruhi atasamehewa. Lakini, atamlipa fidia ya muda alioupoteza kitandani, na kuhakikisha amemwuguza mpaka apone kabisa.

20. “Mtu akimpiga mtumwa wake wa kiume au wa kike kwa fimbo na kumwua papo hapo, ni lazima aadhibiwe.

21. Lakini mtumwa huyo akibaki hai siku moja au mbili, bwana wake hataadhibiwa, kwani huyo alikuwa ni mali yake.

22. “Wanaume wakipigana na kumwumiza mwanamke mjamzito, hata mimba yake ikaharibika bila madhara mengine zaidi, yule aliyemwumiza atatozwa faini kama atakavyodai mumewe mwanamke huyo na kama mahakimu watakavyoamua.

23. Lakini kama yatakuwapo madhara mengine, basi, lazima amlipe uhai kwa uhai,

24. jicho kwa jicho, jino kwa jino, mkono kwa mkono, mguu kwa mguu,

Kusoma sura kamili Kutoka 21