Agano la Kale

Agano Jipya

Kumbukumbu La Sheria 30:1-12 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Mose akaendelea kusema, “Nimewapeni uchaguzi kati ya baraka na laana. Mambo hayo yote yakiwapata nanyi mkiyatafakari popote mlipo miongoni mwa mataifa ambamo Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu atakuwa amewatawanya,

2. mkamrudia Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, nyinyi na watoto wenu, mkatii kwa moyo wote na roho yote neno lake ninalowaamuru leo,

3. hapo Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, atawarudishieni mema yenu na kuwahurumia na kuwakusanya tena kutoka katika mataifa ambamo atakuwa amewatawanya.

4. Na hata kama mmetawanywa katika sehemu mbali kabisa duniani, Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, atawakusanya na kuwarudisheni,

5. ili muimiliki tena nchi ambamo waliishi wazee wenu. Naye atawafanya mfanikiwe zaidi na kuwa wengi kuliko wazee wenu.

6. Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, atawafanyeni nyinyi na wazawa wenu muwe na moyo wa utii ili mumpende yeye kwa moyo wenu wote na roho yenu yote, mpate kuishi.

7. Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, atazifanya laana hizi zote ziwapate adui zenu ambao waliwatesa.

8. Nanyi mtaitii sauti ya Mwenyezi-Mungu na kuzishika amri zake zote ninazowapeni leo.

9. Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu atawafanya mfanikiwe katika kila mtakalofanya; mtakuwa na watoto wengi na ng'ombe wengi na mashamba yenu yatatoa mazao. Maana atapenda tena kuwafanya mfanikiwe kama vile alivyopenda kuwafanikisha wazee wenu,

10. ikiwa mtiatii sauti yake na kushika amri na masharti yake yaliyoandikwa katika kitabu hiki cha sheria na kumrudia Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, kwa moyo wote na roho yote.

11. “Amri ninazowapa leo si ngumu mno kwenu, wala haziko mbali nanyi.

12. Haziko mbinguni hata mseme, ‘Nani atakayepanda juu mbinguni kutuletea ili tupate kuzisikia na kuzitii?’

Kusoma sura kamili Kumbukumbu La Sheria 30