8. Utaingia nchini Yuda kwa nguvu na kufurika na kupanda mpaka shingoni; utaenea juu ya nchi yako yote, ee Emanueli!”
9. Unganeni enyi watu wa mataifa nanyi mtafedheheshwa!Sikilizeni enyi nchi za mbali duniani!Jiwekeni tayari na kufedheheshwa;naam, kaeni tayari na kufedheheshwa.
10. Shaurianeni pamoja lakini itakuwa bure;fanyeni mipango lakini haitafaulu,maana Mungu yu pamoja nasi.
11. Mwenyezi-Mungu alinionya kwa nguvu nisifuate njia za watu hawa, akaniambia,
12. “Usijumuike nao katika njama zao, wala usiogope yale wanayoyaogopa wala kuwa na hofu.
13. Nitambue mimi peke yangu, Mwenyezi-Mungu wa majeshi, kuwa mtakatifu; utaniogopa na kunicha mimi peke yangu.
14. Mimi nitakuwa kimbilio, nitakuwa pia kama jiwe la kujikwaa, mwamba wa kuziangusha falme za Israeli na Yuda; nitakuwa mtego wa kuwatega na kuwanasa wakazi wa Yerusalemu.
15. Watu wengi watajikwaa, wataanguka na kupondeka; watanaswa katika mtego huo na kuchukuliwa mateka.”
16. Nitalihifadhi agizo hilo na kulifunga fundisho hilo miongoni mwa wafuasi wangu.