Agano la Kale

Agano Jipya

Hesabu 7:79-89 Biblia Habari Njema (BHN)

79. Sadaka yake ilikuwa: Sahani moja ya fedha ya kilo moja u nusu na bakuli la fedha la gramu 800 kadiri ya vipimo vya hema takatifu; sahani na bakuli vikiwa vimejazwa unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya sadaka ya nafaka;

80. kisahani kimoja cha dhahabu cha gramu 110 ambacho kilikuwa kimejazwa ubani;

81. fahali mmoja mchanga, kondoo dume mmoja wa mwaka mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa;

82. beberu mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi;

83. fahali wawili, kondoo madume watano, beberu watano na wanakondoo madume wa mwaka mmoja watano kwa ajili ya tambiko ya sadaka ya amani. Hiyo ndiyo iliyokuwa sadaka ya Ahira mwana wa Enani.

84. Jumla ya matoleo ya sadaka za viongozi wa Israeli kwa ajili ya madhabahu siku ilipowekwa wakfu ilikuwa: Sahani za fedha kumi na mbili, birika za fedha kumi na mbili, na visahani vya dhahabu kumi na viwili.

85. Kila sahani ya fedha, ilikuwa yenye uzito wa kilo moja u nusu na kila kisahani kilikuwa chenye uzito wa gramu 800. Hivyo vyombo vyote vilikuwa na uzito wa kilo ishirini na saba na gramu 600 kadiri ya vipimo vya hema takatifu.

86. Vile visahani vya dhahabu kumi na viwili vyenye kujaa ubani, kila kimoja kikiwa na uzito wa gramu 110 kadiri ya vipimo vya hema takatifu vilikuwa na jumla ya uzito wa kilo moja na gramu 320.

87. Jumla ya wanyama wote wa sadaka ya kuteketezwa ilikuwa mafahali kumi na wawili, kondoo madume kumi na wawili, na wanakondoo madume wa mwaka mmoja kumi na wawili, pamoja na sadaka ya nafaka na beberu kumi na wawili kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi,

88. na kwa ajili ya tambiko ya sadaka ya amani, jumla ya wanyama waliotolewa ilikuwa mafahali ishirini na wanne, kondoo madume sitini, beberu sitini, na wanakondoo madume wa mwaka mmoja sitini. Hiyo ndiyo iliyokuwa sadaka iliyotolewa kwa ajili ya madhabahu, baada ya madhabahu hiyo kupakwa mafuta.

89. Wakati Mose alipoingia ndani ya hema la mkutano ili kuongea na Mwenyezi-Mungu, alisikia sauti kutoka upande wa juu wa kiti cha rehema, kilichokuwa juu ya sanduku la agano, kutoka kati ya wale viumbe wawili wenye mabawa.

Kusoma sura kamili Hesabu 7