Agano la Kale

Agano Jipya

Hesabu 4:2-16 Biblia Habari Njema (BHN)

2. “Wahesabu watu wa ukoo wa Kohathi, mmoja wa koo za Lawi, kufuatana na jamaa zao na koo zao;

3. utawaorodhesha wanaume wote wenye umri kati ya miaka thelathini na hamsini wanaofaa kujiunga na huduma ya hema la mkutano.

4. Hii ndio itakayokuwa huduma ya wana wa Kohathi, kuhusu vitu vitakatifu kabisa.

5. “Wakati wa kuvunja kambi, Aroni na wanawe wataingia katika hema, na kulishusha pazia lililoko mbele ya sanduku la agano, kisha walifunike kwa pazia hilo.

6. Juu yake wataweka kifuniko cha ngozi laini ya mbuzi, kisha watatandaza kitambaa cha rangi ya buluu safi. Halafu wataingiza mipiko ya kulichukulia sanduku hilo.

7. “Juu ya meza ya kutolea mikate inayowekwa mbele ya Mwenyezi-Mungu watatandaza kitambaa cha buluu ambacho juu yake wataweka sahani, visahani vya ubani, bakuli na bilauri, kwa ajili ya kutolea tambiko za kinywaji. Daima kutakuwa na mkate juu ya meza.

8. Kisha, watavifunika vyombo hivi vyote kwa kitambaa chekundu, na juu yake wataweka kifuniko cha ngozi laini ya mbuzi. Halafu wataingiza mipiko yake ya kulibeba.

9. “Watachukua kitambaa cha buluu ambacho watafunikia kinara cha taa na taa zake, makasi zake, sinia zake na vyombo vyote vinavyotumiwa kukiwekea mafuta.

10. Watakiweka pamoja na vyombo vyake vyote ndani ya ngozi laini ya mbuzi na kukiweka juu ya mipiko ya kuchukulia.

11. “Halafu watatandaza kitambaa cha buluu juu ya madhabahu ya dhahabu na kuifunika kwa ngozi laini ya mbuzi juu yake. Halafu wataingiza mipiko yake ya kuichukulia.

12. Watavichukua vyombo vyote vinavyotumika mahali patakatifu, watavifunga kwa kitambaa cha buluu na kuvifunika kwa ngozi laini ya mbuzi, kisha wataviweka juu ya mipiko yake ya kuchukulia.

13. Watayaondoa majivu kutoka madhabahuni na juu yake watatandaza kitambaa cha zambarau.

14. Juu yake wataviweka vyombo vyote vitumikavyo katika ibada kwenye madhabahu: Vyetezo, nyuma, miiko na mabakuli. Kisha, juu yake watatandaza kifuniko cha ngozi laini ya mbuzi na kuiingiza mipiko yake ya kulibebea.

15. Baada ya Aroni na wanawe kupafunika mahali patakatifu pamoja na vyombo na vifaa vyake vyote, wakiwa tayari kuanza safari, watu wa ukoo wa Kohathi watakuja na kuvibeba. Lakini wao, hawaruhusiwi kabisa kuvigusa vyombo hivyo vitakatifu, wasije wakafa. Hiyo ndiyo kazi ya ukoo wa Kohathi kila wakati hema la mkutano linapohamishwa.

16. Eleazari mwana wa kuhani Aroni itampasa kuyatunza mafuta ya taa, ubani wa kunukia, tambiko za nafaka za kila siku, mafuta ya kupaka ili kuweka wakfu na kila kitu kilichowekwa wakfu katika hema hilo.”

Kusoma sura kamili Hesabu 4