Agano la Kale

Agano Jipya

Hesabu 31:5-19 Biblia Habari Njema (BHN)

5. Basi, watu 1,000 walitolewa kutoka kila kabila miongoni mwa maelfu ya Waisraeli, jumla wanaume 12,000 wenye silaha.

6. Mose aliwapeleka vitani chini ya uongozi wa Finehasi mwana wa kuhani Eleazari, akiwa na vyombo vya mahali patakatifu na tarumbeta za kutoa ishara.

7. Waliishambulia nchi ya Midiani, kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose, wakawaua wanaume wote.

8. Miongoni mwa watu hao waliouawa, kulikuwako wafalme watano wa Midiani: Evi, Rekemu, Suri, Huri na Reba. Vilevile walimuua Balaamu mwana wa Beori.

9. Waisraeli waliteka nyara: Ng'ombe, kondoo na mali yao yote.

10. Miji yao yote, makazi yao na kambi zao zote waliziteketeza kwa moto.

11. Walichukua nyara zote na mateka yote, ya watu na ya wanyama,

12. wakampelekea Mose na Eleazari, na jumuiya yote ya Waisraeli iliyokuwa kambini katika nchi tambarare za Moabu, ngambo ya Yordani karibu na Yeriko.

13. Mose, kuhani Eleazari, na viongozi wote wa jumuiya ya Waisraeli walitoka kambini, wakaenda kuwalaki wanajeshi.

14. Mose alikasirishwa na maofisa wa jeshi na makamanda waliosimamia makundi ya majeshi 1,000 na makundi ya wanajeshi mamia waliorudi kutoka vitani.

15. Mose akawauliza, “Kwa nini mmewaacha wanawake hawa wote hai?

16. Kumbukeni kwamba wanawake ndio waliofuata shauri la Balaamu, wakasababisha Waisraeli wamwasi Mwenyezi-Mungu kule Peori hata maradhi mabaya yakawajia watu wake Mwenyezi-Mungu.

17. Kwa hiyo basi, waueni watoto wote wa kiume na kila mwanamke aliyewahi kulala na mwanamume.

18. Lakini msiwaue wasichana wote ambao hawajapata kulala na mwanamume; waacheni hai kwa ajili yenu wenyewe.

19. Wote wale walio miongoni mwenu ambao wameua mtu au kugusa maiti ni lazima wakae nje ya kambi kwa muda wa siku saba; jitakaseni pamoja na mateka wenu katika siku ya tatu na ya saba.

Kusoma sura kamili Hesabu 31